Select Page

Masomo ya Misa Mei 3

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 03/05/2024

2024 MEI 3 : IJUMAA-JUMA LA TANO LA PASAKA

WAT. FILIPO NA YAKOBO, MITUME
Rangi: Nyekundu
Zaburi: Juma 1

Somo 1. 1 Kor 15:1-8

Ndugu zangu, nawaarifu ile Injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri; isipokuwa mliamini bure. Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alimtokea Kefa; tena na wale Thenashara; baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja; katika hao wengi wanaishi hata sasa, ila baadhi yao wamelala; baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote; na mwisho wa watu wote, alinitokea mimi, kama ni mtu aliyezaliwa si kwa wakati wake.

Wimbo wa Katikati. Zab 19:2-5

“1. Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu,
Na anga laitangaza kazi ya mikono yake.
Mchana husemezana na mchana,
Usiku hutolea usiku maarifa. (K)

K) Sauti yao imeenea duniani mwote.

2. Hakuna lugha wala maneno,
Sauti yao haisikilikani.
Sauti yao imeenea duniani mwote,
Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.
Katika hizo ameliwekea jua hema. (K)”

Injili. Yn 14:6-14

Yesu alimwambia Tomaso: Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba, tangu sasa mnamjua, tena mmemwona. Filipo akamwambia, Bwana, utuoneshe Baba, yatutosha. Yesu akamwambia, Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe wasemaje, Utuoneshe Baba? Husadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu? Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake. Mnisadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu; la! hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe. Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba. Nanyi mkiomba lolote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana. Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya.

SALA: Ee Yesu naomba unifungue macho yangu ya imani nimwone Baba kupitia wewe.

TAFAKARI

YESU NI NJIA YETU: Leo tunaadhimisha sikukuu ya watakatifu Filipo na Yakobo mitume. Hawa walitambua umuhimu wa maisha ya sadaka ili waweze kufika kwa Baba. Katika Injili tunaona kuwa Yesu ni Sakramenti ya Baba, yaani tunamwona Baba kupitia Yesu. Yesu anaposema yeye ni njia ya kwenda kwa Baba, hamaanishi kuwa yeye ni barabara tu bali anayetaka kwenda kwa Baba ni lazima aishi na kutenda kama Yesu. Yeye ni njia kwa kuwa yeye ndiye mlango wa kuingia na kutoka (Yn 10:9). Yeye ndiye ukweli kwani kwa kumtazama yeye tunamwona Baba. Yeye ni uzima kwani kwa kuishi kama yeye tunaungana na Baba anayetupa uzima. Swali la Philipo la kutamani kumwona Baba liwe tamanio letu sote ila tusimtafute Baba nje ya Yesu. Tumwone Baba katika Neno lake, katika Sakramenti zake, katika mamlaka funzi ya kanisa na katika nafsi ya kuhani mwadhimishaji wa mafumbo matakatifu ya imani yetu. Pia tumwone Baba katika mapokeo matakatifu yanayofunuliwa kwetu na Yesu Kristo.

Masomo ya Misa Mei 2

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 01/05/2024

2024 MEI 1 : JUMATANO-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Atanasi, Askofu na Mwalimu wa Kanisa
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 1

MTAKATIFU ATANASI WA ALEKSANDRIA

by Claretian Publications

Somo 1. Mdo 15:7-21

Wakati wa mtaguso wa Yerusalemu, baada ya hoja nyingi Petro alisimama, akawaambia, Ndugu zangu, ninyi mnajua ya kuwa tangu siku za kwanza Mungu alichagua miongoni mwenu ya kwamba Mataifa walisikie neno la Injili kwa kinywa changu na kuliamini. Na Mungu, ajuaye mioyo ya watu, akawashuhudia, akiwapa Roho Mtakatifu vile vile kama alivyotupa sisi; wala hakufanya tofauti kati yetu sisi na wao, akiwasafisha mioyo yao kwa imani. Basi sasa mbona mnamjaribu Mungu na kuweka kongwa juu ya shingo za wanafunzi, ambalo baba zetu wala sisi hatukuweza kulichukua. Bali twaamini kwamba tutaokoka kwa neema ya Bwana Yesu vile vile kama wao. Basi mkutano wote wakanyamaza, wakawasikiliza Barnaba na Paulo wakiwapasha habari za ishara na maajabu, ambayo Mungu aliyafanya kwa ujumbe wao katika Mataifa. Na hao walipokwisha kunyamaza Yakobo akajibu, akisema, Ndugu zangu, nisikilizeni. Simeoni ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya manabii yapatana na hayo, kama ilivyoandikwa. Baada ya mambo haya nitarejea, nami nitaijenga tena nyumba ya Daudi iliyoanguka. Nitajenga tena maanguko yake, nami nitaisimamisha; ili wanadamu waliosalia wamtafute Bwana, na mataifa yote ambao jina langu limetajwa kwao; asema Bwana, ajulishaye hayo tangu milele. Kwa sababu hiyo mimi naamua hivi; tusiwataabishe wale waliomgeukia Mungu katika mataifa; bali tuwaandikie kwamba wajiepushe na unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa, na damu. Kwa maana tangu zamani za kale Musa anao watu wahubirio mambo yake; katika kila mji husomwa kila Sabato katika masinagogi.

(K) Wahubirini mataifa habari za utukufu wake.

Wimbo wa Katikati. Zab 96:1-3, 10

“1. Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Mwimbieni Bwana nchi yote.
Mwimbieni Bwana, libarikini jina lake. (K)

2. Tangazeni wokovu wake siku kwa siku.
Wahubirini mataifa habari za utukufu wake,
Na watu wote habari za maajabu yake. (K)

3. Semeni katika mataifa, Bwana ametamalaki;
Naam, ulimwengu umethibitika usitikisike,
Atawahukumu watu kwa adili. (K) “

Injili. Yn 15:9-11

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Kama vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe.

TAFAKARI

UPENDO NI UKAMILIFU WA FURAHA YOTE: Upendo ni fadhila ya Kimungu inayotuwezesha kumpenda Mungu kuliko vitu vingine vyote na kumpenda jirani kama Kristo alivyotupenda. Katika Injili ya leo Yesu anatufundisha kuwa furaha ya kweli ipo katika kushika amri zake hususani amri ya upendo. Utambulisho wa Mkristo unapaswa kuoneshwa kwa njia ya upendo wa kweli. Kipimo cha upendo wa kweli ni Yesu mwenyewe na siyo mwanadamu. Agano la Kale linatufundisha kumpenda jirani kama nafsi (rej. Wal 19:1). Yesu anakamilisha amri hii kwa kutuonesha kuwa kipimo cha upendo wa kweli ni yeye. Kama alivyompenda Baba, nasi hatuna budi kupendana, vivyo hivyo. Upendo wa kweli unaweza kutenda mambo makubwa. Tushirikishane upendo wa Kristo kwa kuwajali wahitaji na kuwapatia mahitaji yao. Wajane Yatima, Wagane, Wagonjwa, Wafungwa ni makundi yanayotegemea kupata upendo wa pekee kutoka kwetu.

SALA: Ee Yesu naomba uniwashie fadhila ya mapendo.

Masomo ya Misa Mei 1

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 01/05/2024

2024 MEI 1 : JUMATANO-JUMA LA TANO LA PASAKA

MT. YOSEFU MFANYAKAZI
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 1

SOMO I: Mwa. 1:26-2:3

Mungu alisema, Na tufanye mtu kwa mfano wetu; kwa sura yetu; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kila chenye kutambaa kitambaacho juu ya nchi. Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi. Mungu akasema, tazama, nimewapa kila mche utoao mbegu, uliojuu ya uso wa nchi yote pia, na kila mti ambao matunda yake yana mbegu; vitakuwa ndivyo chakula chenu; na chakula cha kila mnyama wa nchi, na cha kila ndege wa angani, na cha kila kitu kitambaacho juu ya nchi, chenye uhai; majani yote ya miche ndiyo chakula chenu; ikawa hivyo. Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya sita. Basi mbingu na nchi zikamalizika, na jeshi lake lote. Na siku ya saba Mungu alimaliza kazi yake yote aliyoifanya; akastarehe siku ya saba, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoifanya. Mungu akaibarikia siku ya saba, akaitakasa kwa sababu katika siku hiyo Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya.

 Zab. 90:2- 4, 12-14, 16

1. Kabla haijazaliwa milima, wala hujaiumba dunia,
Na tangu milele hata milele ndiwe Mungu.

2. Wamrudisha mtu mavumbini,
Usemapo, Rudini, enyi wanadamu.
Maana mika elfu machoni pako
Ni kama siku ya jana ikiisha kupita,
Na kama kesha la usiku. (K)

3. Basi, utujulishe kuzihesabu siku zetu,
Tujipatie moyo wa hekima.
Ee Bwana urudi, hata lini?
Uwahurumie watumishi wako. (K)

4. Utushibishe asubuhi kwa fadhili zako,
Nasi tutashangilia na kufurahi siku zetu zote.
Utufurahishe kwa kadiri ya siku ulizotutesa,
Kama miaka ile tuliyoona mabaya.
Matendo yako na yaonekane kwa watumishi wako. (K)

(K) Kazi ya mikono yetu uithibitishe, Ee Bwana.

INJILI: Mt. 13:54-58
Yesu alipofika nchi yake, akawafundisha makutano katika sinagogi lao, hata wakashangaa, wakasema, Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii? Huyu si mwana wa seremala? mamaye si yeye aitwaye Mariamu? Na nduguze si Yakobo, naYusufu, na Simoni, na Yuda? Na maumbu yake wote hawapo hapa petu? Basi huyu amepata wapi haya yote? Wakachukizwa naye. Yesu akawaambia, Nabii hakosi kupata heshima, isipokuwa katika nchi yake, na nyumbani mwake mwenyewe. Wala hakufanya miujiza mingi huko, kwa sababu ya kutokuamini kwao.

TAFAKARI

TUACHE KUMTESA YESU: Katika somo la kwanza, tunaona ukuu wa neema ya Mungu. Neema hii ilifanya mambo ambayo nivigumu kuyaelewa kabisa. Kumvua aliyekuwa mtesi wa Kanisa kuwa mlinzi wa Kanisa. Saulo alikuwa akimtesa Kristo kwa kulitesa kanisa. Hii ni kwa sababu Kanisa ni mwili wa kichwa cha Kristo (1Kor 12:27). Mara ngapi na mimi ninalitesa Kanisa? Katika hili, labda kwa baadhi yetu ni zaidi ya Paulo. Ni mara ngapi nimelisema Kanisa vibaya, ni mara ngapi nimelichafua Kanisa kwa matendo yangu maovu kama ulevi, ushirikina na uasherati? Ni mara ngapi nimekataa kulipa zaka. Kweli baadhi yetu ni zaidi ya Paulo. Leo tunapomkumbuka Yosefu mfanyakazi, tuombe moyo wa kujitolea kwa ajili ya kazi ya Bwana. Yeye alisifika kwa kujitolea. Tumfariji Kristo kwa kujitolea zaidi kwa kazi ya Bwana. Tuache kumuumiza kristo. Tuanze upya na Kristo Mfufuka.

Sala: Ee Yesu ninakuomba unihurumie kwa kushiriki katika kukutesa wewe.

Masomo ya Misa Aprili 30

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 30/04/2024

2024 APRILI 30 : JUMANE-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Pio V, Papa
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 1

Somo 1. Mdo 14:19-28

Wayahudi walifika toka Antiokia na Ikonio, wakawashawishi makutano hata wakampiga kwa mawe Paulo, wakamburuta nje ya mji, wakidhani ya kuwa amekwisha kufa. Lakini wanafunzi walipokuwa wakimzunguka pande zote, akasimama, akaingia ndani ya mji; na siku ya pili yake akatoka, akaenda zake pamoja na Barnaba mpaka Derbe. Hata walipokwisha kuhubiri Injili katika mji ule, na kupata wanafunzi wengi, wakarejea mpaka Listra na Ikonio na Antiokia, wakifanya imara roho za wanafunzi na kuwaonya wakae katika ile imani, na ya kwamba imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi. Na walipokwisha kuwachagulia wazee katika kila kanisa, na kuomba pamoja na kufunga, wakawaweka katika mikono ya Bwana waliyemwamini. Wakapita kati ya Pisidia wakaingia Pamfilia. Na baada ya kuhubiri lile neno katika Perge wakatelemka mpaka Atalia. Na kutoka huko wakaabiri kwenda Antiokia. Huko ndiko walipoombewa neema ya Mungu kwa ile kazi waliyokwisha kuitimiza. Hata walipofika wakalikutanisha kanisa, wakawaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nao, na ya kwamba amewafungulia mataifa mlango wa imani. Wakaketi huko wakati usiokuwa mchache, pamoja na wanafunzi.

(K). Watawajulisha watu matendo yake makuu, Na utukufu wa fahari wa zamani zote. 

Wimbo wa Katikati. Zab 145:10-13, 21

“1. Ee Bwana, kazi zako zote zitakushukuru,
Na wacha Mungu wako watakuhimidi.
Wataunena utukufu wa ufalme wako,
Na kuuhadithia uweza wako,
Ili kuwajulisha watu matendo yake makuu,
Na utukufu wa fahari ya ufalme wake. (K)

2. Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote,
Na mamlaka yako ni ya vizazi vyote. (K)

3. Kinywa change kitazinena sifa za Bwana;
Wote wenye mwili na walihimidi jina lake takatifu
milele na milele. (K)”

Injili. Yn 14:27-31

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Amani nawaachieni; amani yangu nawapa; niwapavyo mimi sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga. Mlisikia ya kwamba mimi naliwaambia, Naenda zangu, tena naja kwenu. Kama mngalinipenda, mngalifurahi kwa sababu naenda kwa Baba; kwa maana Baba ni mkuu kuliko mimi. Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu. Lakini ulimwengu ujue ya kuwa nampenda Baba; na kama vile Baba alivyoniamuru; ndivyo nifanyavyo. Ondokeni, twendeni zetu.

TAFAKARI

KRISTO NI AMANI YETU YA KWELI: Yesu anawaachia wafuasi wake kati ya zawadi kubwa za kipasaka: Amani. Kristo anajitofautisha na dunia hata katika kutoa amani. Yeye anatuachia amani ambayo dunia haiwezi kuitoa. Amani ya dunia hii ni ya muda, ndio maana mpaka leo dunia inashuhudia vurugu sehemu mbalimbali. Amani ya dunia hii ni ya mkataba; tumeshuhudia nchi kadhaa zikiwekeana saini za mikataba ya amani, na mara mikataba hii inapovunjika, na amani nayo huvunjika. Amani ya dunia hii mara kadhaa hupatikana baada ya mtutu wa bunduki. Na hii si amani ambayo Kristo anaichia dunia. Kristo dunia amani ambayo imepatikana kwa njia ya Damu yake iliyomwagika pale msalabani. Amani hiyo ni ya kudumu. Ni amani iletayo faraja ya roho na mwili. Ni amani ile ambayo ni tunda la Roho Mtakatifu; amani ambayo iliwafariji wafuasi wa kwanza wakati wa mateso katika kuhubiri Habari njema kama tusomavyo katika somo la kwanza kwamba “Imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi”(Mdo 14:22).

SALA: Ee Kristo Mfufuka uijalie dunia amani ya kweli. 

Masomo ya Misa Aprili 29

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 29/04/2024

2024 APRILI 29 : JUMATATU-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Katarina wa Siena, Bikira, Mwalimu wa Kanisa
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 1

Somo 1. Mdo 14:5-18

Siku zile, palipotokea shambulio la watu wa Mataifa na Wayahudi pamoja na wakubwa wao juu yao, kuwatenda jeuri na kuwapiga kwa mawe, wao wakapata habari wakakimbilia Listra na Derbe, mji wa Likaonia, na nchi zilizo kando kando; wakakaa huko, wakiihubiri Injili. Na huko Listra palikuwa na mtu mmoja, dhaifu wa miguu, kiwete tangu tumboni mwa mamaye, ambaye hajaenda kabisa. Mtu huyo alimsikia Paulo alipokuwa akinena; ambaye akamkazia macho na kuona ya kuwa ana imani ya kuponywa, akasema kwa sauti kuu, Simama kwa miguu yako sawasawa. Akasimama upesi akaenda. Na makutano walipoona aliyoyafanya Paulo wakapaza sauti zao, wakisema kwa Kilikaonia, Miungu wametushukia kwa mifano ya wanadamu. Wakamwita Barnaba, Zeu, na Paulo, Herme, kwa sababu ndiye aliyekuwa mnenaji. Kuhani wa Zeu ambaye hekalu lake lilikuwa mbele ya mji, akaleta ng’ombe na taji za maua hata malangoni, akitaka kutoa dhabihu pamoja na makutano. Walakini mitume Barnaba na Paulo, walipopata habari, wakararua nguo zao, wakaenda mbio wakaingia katika makutano, wakipiga kelele, wakisema, Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi ni wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; ambaye zamani zilizopita aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe. Lakini hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha. Na kwa maneno hayo wakawazuia makutano kwa shida, wasiwatolee dhabihu.

(k) Ee Bwana, kutukuza usitutukuze sisi, Bali ulitukuze jina lako. 

Claret Catholic Center: Kwa mahitaji mbalimbali ya vifaa vya Makanisani na  Zawadi za waamini. Tupigie/whatsapp 255 688 404 040

Wimbo wa Katikati. Zab 115:1-4, 15-16

“1. Ee Bwana, kutukuza usitutukuze sisi,
Bali ulitukuze jina lako.
Kwa ajili ya fadhili zako,
Kwa ajili ya uaminifu wako.
Kwa nini mataifa kusema,
Yuko wapi Mungu wao? (K)

2. Lakini Mungu wetu yuko mbinguni,
Alitakalo lote amelitenda
Sanamu zao ni fedha na dhahabu,
Kazi ya mikono ya wanadamu. (K)

3. Na mbarikiwe ninyi na Bwana,
Aliyezifanya mbingu nan chi.
Mbingu ni mbingu za Bwana,
Bali nchi amewapa wanadamu. (K)”

Injili. Yn 14:21-26

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda na kujidhihirisha kwake. Yuda (siye Iskariote), akamwambia, Bwana, imekuwaje ya kwamba wataka kujidhihirisha kwetu, wala si kwa ulimwengu? Yesu akajibu, akamwambia, Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake. Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka. Hayo ndiyo niliyowaambia wakati nilipokuwa nikikaa kwenu. Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.

SALA: Tuombe Mungu atupe moyo wa kujishusha na kuwa wanyenyekevu.

TAFAKARI

SIFA NA UTUKUFU NI KWA MUNGU: Yesu amesema katika Injili “yeye aliye na amri zangu atapendwa na Baba yangu.” Imani yetu lazima ijikite katika kumtukuza Mungu na sio katika kujitukuza sisi wenyewe. Ndio maana hata katika somo la kwanza, baada ya akina Barnaba na Paulo kumponya yule kiwete, alipotaka kuwarudishia shukrani na kuonesha kuwa ni wao waliomponya, tunaona mitume wanakataa na kuoneshsa kuwa ni Mungu. “Akina Bwana mbona mnafanya haya? Sisi nasi ni wanadamu kama nyie.” Hapa ni dhihirisho tosha kuwa Mungu ndiye mtendaji mkuu wa hiyo miujiza na si wao. Ni katika hili Yesu alionesha kuwa tujifungamanishe na yeye na Baba ili wafanye maskani/makao kwetu, tusijitukuze katika utume wetu. Wapo watu ambao wanasubiri kusifiwa na kutukuzwa kwa wanavyofanya utume, wanatamani wawe miungu mtu. Kwa hali hii wanachukua nafasi ya Mungu. Hawako tayari kurarua nguo zao na kujishusha kama walivyofanya mitume.

Masomo ya Misa Aprili 28

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 28/04/2024

2024 APRILI 28 : DOMINIKA YA TANO YA PASAKA

Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 1

Somo 1. Mdo 9: 26-31

Sauli alipofika Yerusalemu, alijaribu kujiunga na wanafunzi, nao walikuwa wakimwogopa wote, wasisadiki ya kuwa yeye ni mwanafunzi. Lakini Barnaba akamtwaa, akampeleka kwa mitume akawaeleza jinsi alivyomwona Bwana njiani, na ya kwamba alisema naye, na jinsi alivyohubiri kwa ushujaa katika Dameski kwa jina lake Yesu. Naye akawa pamoja nao katika Yerusalemu akiingia na kutoka. Akahubiri kwa jina la Bwana kwa ushujaa, akinena na kuhojiana na Wayahudi wa Kiyunani. Nao wakajaribu kumwua. Lakini ndugu walipopata habari wakamchukua mpaka Kaisaria, wakampeleka aende Tarso. Basi Kanisa likapata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likiendelea na kuongezeka katika kicho cha Bwana, na faraja ya Roho Mtakatifu.

K) Kwako, Bwana, zinatoka sifa zangu katika kusanyiko kubwa. 

Wimbo wa Katikati. Zab 22: 26- 28, 30-32

“1. Nitaziondoa nadhiri zangu
Mbele yao wamchao.
Wapole watakula na kushiba,
Wamtafutao Bwana watamsifu;
Mioyo yenu na iishi milele. (K)

2. Miisho yote ya dunia itakumbuka
Na watu watamrejea Bwana;
Jamaa zote za mataifa watamsujudia.
Wakwasi wote wa dunia watakula na kusujudu,
Humwinamia wote washukao mavumbini. (K)

3. Naam, yeye asiyeweza kujihuisha nafsi yake,
Wazao wake watamtumikia.
Zitasimuliwa habari za Bwana,
Kwa kizazi kitakachokuja,
Nao watawahubiri watakaozaliwa haki yake,
Ya kwamba ndiye aliyefanya. (K)

Somo 2. 1 Yoh 3: 18-24

Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli. Katika hili tutafahamu ya kwamba tu wa kweli, nasi tutaituliza mioyo yetu mbele zake, ikiwa mioyo yetu inatuhukumu; kwa maana Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote. Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu; na lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake. Na hii ndiyo amri yake, kwamba tuliamini jina la Mwana wake Yesu Kristo, na kupendana sisi kwa sisi, kama alivyotupa amri. Naye azishikaye amri zake hukaa ndani yake yeye, naye ndani yake. Na katika hili tunajua ya kuwa anakaa ndani yetu, kwa huyo Roho aliyetupa.

Injili. Yn 15: 1-8

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Mimi ndimi mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. Kila tawi ndani yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa. Ninyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya lile neno nililowaambia. Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi; akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamuwezi kufanya neno lo lote. Mtu asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea. Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa. Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu.

TAFAKARI

“NI KATIKA KRISTO TUTAZAA MATUNDA
Moja ya changamoto inayoikabili jamii ya mwanadamu leo hii ni migawanyiko na ubinafsi kati ya wanadamu. Hali hii ni tishio kwa ustawi wa utu wa mtu na hupambwa na matendo mengi yenye kuungamiza ubinadamu wetu. Kila mmoja anajiamulia kadiri aonavyo inafaa na kujiwekea taratibu za kimaisha zinazoendana na vionjo au mawazo yake. Hivyo unyonyaji, ukiukwaji wa haki za wengine, mauaji, dhuluma na mengine mengi yanaupinga ubinadamu na bila binadamu huyu kujisikia katika dhamiri yake anatenda vibaya dhidi ya ndugu yake. Bila kuwa na chimbuko moja la uhai wetu kimaadili ni aghalabu kuujenga umoja na kuonja athari za migawanyiko hii. Dominika ya leo inatualika jamii nzima ya waamini kujitathimini na kuimarisha umoja wetu unaojijenga katika Kristo Mfufuka. Yeye anajitambulisha kwetu kuwa ni mzabibu ambao matawi yake ni sisi tunaomfuasa. Hivyo tunavyobaki katika mzabibu huo kama matawi na Yeye akiwa shina letu tunatajirishwa na kuuhishwa na yeye na pia kuwa katika hali ya umoja wa kindugu.
Kristo anaanza kwa kujitambulisha kama mzabibu wa kweli: “Mimi ndimi mzabibu wa kweli na Baba yangu ni mkulima.” Yatosha kurejea nyuma na kutafakari taswira ya mzabibu katika Agano la Kale. Taifa la Israeli lilipewa haiba hiyo lakini mara nyingi lilizaa zabibu mwitu (rej. Isa 5:1- 7). Hapa kuna tofauti kati ya mzabibu wa kweli na “mzabibu mwitu”. Mzabibu mwitu unazaa zabibu mwitu ambazo ni chukizo na hazifai kwa matumizi na kinyume chake mzabibu wa kweli huzaa matunda halisi. Umuhimu wa Kristo kama mzabibu unaonekana katika muunganiko wake na Mungu Baba. Yeye aliye shina la mzabibu anachota yote kutoka kwa Baba na hivyo kuweka mbele yetu kipimo kimoja na chanzo kimoja kwa utendaji wetu na uwepo wetu sisi. Kristo anajitambulisha katika taswira ya mzabibu na kutuunganisha sisi katika mzabibu huo kama matawi yake: “nanyi mu matawi yangu.” Matawi haya yataweza kuzaa pale tu yatakapobaki yameungana na tawi. Bila kukaa katika Yeye hatuwezi kuzaa matunda: “kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokuwa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu.”
Dominika iliyopita Kristo alijitanabaisha katika haiba ya Mchungaji Mwema akiwahakikishia Kondoo wake usalama pale wanapokuwa chini ya ulinzi wake (rej. Yn 10:28 -29). Dhana hiyo inaunganika na tafakari ya Dominika hii katika wazo la kuwa na umoja na Kristo. Hakika ya usalama wetu katika Kristo inajifunua au inajidadavua vizuri kwa kuuona na kuutambua umoja tunaoupata kwake kwa njia ya fumbo la umwilisho. Fumbo la umwilisho limetuunganisha na Kristo na matunda yake ni ukombozi wetu wanadamu. Fumbo hili linatuunganisha na Kristo na kwa njia yake tunaunganika sote kama ndugu katika Kristo. Migawanyiko na matendo maovu ya kibinadamu yanayoambatana nayo hupata mwarobaini katika tendo hili. Hivyo mahali popote katika jamii ya mwanadamu kunapoonekana cheche za migawanyiko na matunda yake maovu tunakumbushwa mara moja kumtambua na kumkumbatia Kristo kama mzabibu ambao sisi tulio matawi yake tunapobaki katika yeye na kuungana naye tunazaa matunda ya umoja na upendo katika jamii ya wanadamu. “Kila tawi ndani yangu lisilozaa matunda Baba yangu huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa.” Muunganiko wetu na mzabibu kama matawi kunatudai kutoa matunda. Kwa maneno mengine ukombozi wetu unatutuma katika ushuhuda wa maisha. Imani tunda ambalo linaendelea kukua na kukomaa kila siku.
Somo la pili la Dominika hii linatuelekeza katika hilo na kutuonya katika kutekeleza nyajibu zetu mbalimbali kwa dhamiri iliyo safi, namna ambayo hutufanya kuzaa matunda ya kweli: “Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” Ipo hatari ya kuifurahia au kuifuatilia imani kwa bidii wakati wa faraja na kuikimbia wakati wa madhulumu. Ni changamoto katika kuilinda imani hata kama inahatarisha uhai wako kwa namna yoyote ile. Dhamiri safi ambayo hutusukuma kuzaa matunda mema inatubidisha hata katika hali ya kuwa tayari kutia mchanga kitumbua chako ili mradi umeusimamia ukweli. Maangamizi mengi ya utu wa mtu husababishwa na uzembe wangu au wake katika kutotimiza wajibu tuliopewa inavyotakikana. Nabaki katika ubinafsi wangu na kutojali kuangamia kwa mwenzangu. Najisahau kwamba nimeungana na shina la mzabibu na ninapaswa kuzaa matunda.
Muungano wetu na Kristo kama matawi katika Yeye aliye mzabibu hutupatia hamasa. Hizi ni neema na baraka kutoka mbinguni ambazo kwazo tunachota ujasiri na kukemea au kurekebisha au kusema ukweli kwa ajili ya manufaa ya mwanadamu kadiri ya mapenzi ya Mungu. Huku ndiko kuzaa matunda. Tunaposhindwa kuzaa matunda ukristo wetu unabaki kuwa butu na imani yetu inakosa ladha. Lakini tunapozaa matunda Baba hutusafisha na kuzaa zaidi. Neno la Mungu na mafundisho mbalimbali ya Kanisa hutupatia virutubisho kwa ajili ya kuzaa hayo matunda. Ni namna gani tunajitajirisha na nyenzo hizo ndiyo hakika ya kuzaa matunda mema na mengi. Huwezi kupata zabibu katika michongoma. Jiulize, nini ambacho kwako ni chakula kwa ajili ya roho yako na kuimarisha imani yako? Ni changamoto kubwa sana na hasa katika mazingira ya ulimwengu wa leo wenye teknolojia ya habari na mawasiliano isiyochujwa chini ya mitandao ya kijamii. Tuangalie tusije tukawa ndani ya mzabibu lakini tunakataa au kuzuia kushibishwa na utajiri unaotoka kwake huku tukitegemea kutoka nje ya mzabibu. Kwa hakika tutakakwa na kutupwa nje.
Sauli anakuwa kwetu mfano mzuri wa yeye ambaye ameungana na mzabibu na kuzaa matunda. Ingawa mwanzoni hakupokelewa kwa sababu ya historia yake ya kulidhulumu Kanisa, yeye hakukatishwa tamaa na pia alisaidiwa na utambulisho wa Barnaba. “Akahubiri kwa jina la Bwana kwa ushujaa, akinena na kuhojiana na Wayahudi wa Kiyunani.” Umisionari wetu unatuelekeza katika mambo hayo mawili: kwanza kuhubiri kwa jina la Bwana. Yeye aliye shina letu ndiye chanzo cha yote tuhubiriyo na zaidi Yeye aliye ufunuo wa Baba anatufanya tuyatimize mapenzi ya Baba kwa kuungana naye. Pili ni kuhubiri kwa ushujaa, yaani bila kuogopa na kwa bidii yote. Juhudi ya Sauli inazaa matunda: “Kanisa likapata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likaendelea na kuongezeka katika kicho cha Bwana, na faraja ya Roho Mtakatifu.”
Umoja wetu na Kristo Mfufuka ambaye ni shina la mzabibu udhihirike kwa matendo yetu mema ya kindugu kati yetu sisi kwa sisi. Dominika ya leo tunakumbushwa kurejea na kuwa na shina au chanzo kimoja ambacho kinatoa maana ya maisha yetu kiroho na kimaadili. Yeye ni Kristo Mzabibu wa kweli. Ni mwaliko wa kuinuia macho na kuona umuhimu wa Mwenyezi Mungu katika maisha yangu na hivyo kuimba kama Mzaburi anayesema: “Kwako Bwana, zinatoka sifa zangu katika kusanyiko kubwa.” Hapa tutaweza kweli kuwa wamoja katika Kristo na aliye Njia, Ukweli na Uzima wetu (rej. Yn 14:6). Muunganiko wetu na Kristo kama shina la mzabibu wa kweli unatupatia fursa ya kushibishwa kwa pamoja kwa njia yake na hivyo kuifunua mioyo yetu kwa ajili ya wenzetu.”

SALA: Ee Yesu utupe neema ya kuungana nawe zaidi.