Select Page

Masomo ya Misa julai 27

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 27/07/2024

2024 JULAI 27: JUMAMOSI-JUMA  LA 16 LA MWAKA

Wat. Aurelio na Natalia, Wafiadini
Rangi: Nyeupe

Zaburi: Tazama Sala ya Siku

Soma 1. Yer 7:1-11

Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, simama langoni pa nyumba ya Bwana, ukatangaze hapo neno hili, ukisema, sikilizeni neno la Bwana, ninyi nyote wa Yuda, mnaoingia katika malango haya ili kumwabudu Bwana.Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, tengenezeni njia zenu, na matendo yenu, nami nitawakalisha ninyi mahali hapa. Msitumainie maneno ya uongo, mkisema, Hekalu la Bwana, Hekalu la Bwana, Hekalu la Bwana ndiyo haya. Maana kama mkitengeneza kabisa njia zenu na matendo yenu; kama mkihukumu hukumu ya haki kati ya mtu na jirani yake; kama hamwonei mgeni wala yatima, wala mjane, wala kumwaga damu isiyo na hatia mahali hapa, wala kuifuata miungu mingine kwa hasara yenu wenyewe; ndipo nitakapowakalisha mahali hapa, katika nchi hii niliyowapa baba zenu, tokea zamani hata milele. Angalieni, mnatumainia maneno ya uongo, yasiyoweza kufaidia. Je! Mtaiba, na kuua, na kuzini, na kuapa kwa uongo, na kumfukuzia Baali uvumba, na kuifuata miungu mingine ambayo hamkuijua; kisha mtakuja na kusimama mbele zangu katika nyumba hii, iitwayo kwa jina langu, na kusema, tumepona; ili mpate kufanya machukizo hayo yote? Je! Nyumba hii, iitwayo kwa jina langu, imekuwa pango la wanyang’anyi machoni penu? Angalieni, mimi, naam, mimi, nimeliona jambo hili, asema Bwana.

Wimbo wa Katikati. Zab 84:3-6, 8, 11

1. Nafsi yangu imezionea shauku nyua za Bwana,
Naam na kuzikondea.
Moyo wangu na mwili wangu,
Vinamlilia Mungu aliye hai.

(K) “Maskani zako zapendeza kama nini,
ee Bwana wa majeshi.”

2. Shomoro naye ameona nyumba,
Na mbayuwayu amejipatia kioto,
Alipoweka makinda yake.
Kwenye madhabahu zako, ee Bwana wa majeshi,
Mfalme wangu na Mungu wangu. (K)

3. Heri wakaao nyumbani mwako
Wanakuhimidi daima.
Heri ambaye nguvu zake zatoka kwako,
Na njia ziendazo Sayuni zimo moyoni mwake. (K)

4. Huendelea toka nguvu hata nguvu,
Huonekana Sayuni kila mmoja mbele za Mungu.
Hakika siku moja katika nyua zako
Ni bora kuliko siku elfu.
Ningependa kuwa awabu
Nyumbani mwa Mungu wangu,
Kuliko kukaa hema za uovu. (K)

Injili. Mt 13:24-30

Yesu aliwatolea makutano mfano akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake; lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake. Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu. Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? Limepata wapi basi magugu? Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi.  Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye? Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing’oa ngano pamoja nayo. Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu.

TAFAKARI

MUNGU ANATUPATIA MUDA WA KUBADILI MIENENDO YETU: Katika sehemu ya somo la Injili ya leo mfano tunaopewa wa ngano na magugu unamhusu kila mmoja wetu. Tunapoishi tunaishi kama ngano au gugu? Baada ya maisha ya hapa duniani kila mmoja atajihukumu kulingana na jinsi alivyoishi hapa duniani. Tukiifuata vizuri njia ya Kristo, wakati wa mavuno tutakusanywa katika kundi lake la Ufalme wa Mbinguni. Mtu akishawishika na shetani akipanda uovu katika maisha yake atafananishwa na gugu ambalo halimfurahishi Mungu na siku ya mavuno hutengwa na ngano safi. Ila Mungu ni mwingi wa huruma na Upendo amemwekea mwanadamu muda wa kutosha kujitathimi na kufanya mabadiliko katika maisha yake. Katika somo la kwanza nabii Yeremia amelitaja hilo vizuri anaposema “Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, tengenezeni njia zenu, na matendo yenu, nami nitawakalisha ninyi mahali hapa.” Ndivyo Kristo anavyomfundisha mwanadamu mwenye utashi kwamba akiweza kujitathmini na kutubu atapokea huruma ya Mungu. 

Sala: Ee Bwana Neema yako ituwezeshe kutambua tunapokosea na kufanya toba.

Masomo ya Misa Julai 26

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 26/07/2024

2024 JULAI 26: IJUMAA-JUMA  LA 16 LA MWAKA

Wat. Yoakim na Anna, Wazazi wa Bikira Maria
Rangi: Nyeupe

Zaburi: Tazama Sala ya Siku

SOMO 1:        YbS  44:1, 10-15

Haya na tuwasifu watu wa utauwa, na baba zetu katika vizazi vyao. Lakini hawa walikuwa watu wa utauwa, wala kazi zao za haki hazisahauliki. Wema wao utawadumia wazao wao, na urithi wao una wana wa wana; wazao wao wanashikamana na agano, na watoto wao kwa ajili yao. Kumbukumbu lao litadumu milele, wala haki yao haifutiki kamwe; miili yao imezikwa katika amani, na jina lao laishi hata vizazi vyote. Mkutano wa watu wataitangaza hekima yao, na makusanyiko watazihubiri sifa zao.

Wimbo wa Katikati. Zab. 132: 11, 13-14, 17-18

Bwana amemwapia Daudi neno la kweli, Hatarudi nyuma akalihalifu, Baadhi ya wazao wa mwili wako Nitawaweka katika kiti chako cha enzi.

(K) Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake.

Kwa kuwa Bwana ameichagua Sayuni, Ameitamani akae ndani yake. Hapo ndipo mahali pangu pa raha milele, Hapo nitakaa kwa maana nimepatamani. (K)

Hapo nitamchipushia Daudi pembe, Na taa nimemtengenezea masihi wangu. Adui zake nitawavika aibu, Bali juu yake taji yake itasitawi. (K)

Injili. Mt.  13:16-17

Yesu aliwaambia wanafunzi wake:  Heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia.  Kwa maana, amin, nawaambia, Manabii wengi na wenye haki walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi, wasiyaone; na kuyasikia mnayoyasikia ninyi, wasiyasikie.

TAFAKARI

TUOMBE KUWA NA MACHO NA  MASIKIO YA KIROHO: Leo tunafanya kumbukumbu ya watakatifu Yoakim na Anna, wazazi wa Bikira Maria. Ni kutokana na mapokeo na mafundisho ya Kanisa kuwa wazazi wa mama yetu Maria ni Yoakim na Anna. Umuhimu huu wa Watakatifu Yoakim na Anna unatokana na uhusiano wao na mama yetu Maria na mwanae Yesu. Hawa ni bibi na babu wa Yesu, ni kati ya wanaotengeneza familia kubwa ya Kristo na ndio hawa wanaotupatia Kristo na mama yake Maria. Wazazi hawa ni mfano wa wazazi wenye imani kwa Mungu na wenye kuishi maisha ya familia kwa upendo na uwajibikaji. Kutoka Injili Kristo anasema ‘heri macho yenu kwa kuwa yanaona na masikio yenu kwa kuwa yanasikia.’ Haitoshi tu kuwa na macho haya ya kawaida, ila tumwombe Mungu atujalie macho na masikio ya kiroho. Macho na masikio ya kiroho ndiyo yale yanayotuwezesha kuona kuwa familia yetu ni kubwa ikihusisha pia Yoakim na Anna, na masikio ya Kiroho ni yale yanayotuwezesha kusikia na kuishi mafundisho ya Kristo.

Sala: Ee Kristo, tujalie tuwe na macho na masikio ya kiimani ili maisha yetu yachorwe na upendo wako. Amina.

Masomo ya Misa Julai 25

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 25/07/2024

2024 JULAI 25: ALHAMISI-JUMA  LA 16 LA MWAKA

MT. YAKOBO, MTUME
Rangi: Nyekundu

Zaburi: Tazama Sala ya Siku

Somo 1. 2 Kor 4:7-15

Tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu. Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi; siku zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu. Kwa maana sisi tulio hai, siku zote twatolewa tufe kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu ipatikanayo na mauti. Basi hapo mauti hufanya kazi ndani yetu, bali uzima ndani yenu. Lakini kwa kuwa tuna roho ile ile ya imani; kama ilivyoandikwa, naliamini, na kwa sababu hiyo nalinena; sisi nasi twaamini, na kwa sababu hiyo twanena; tukijua ya kwamba yeye aliyemfufua Bwana Yesu atatufufua sisi nasi pamoja na Yesu, na kutuhudhurisha pamoja nanyi. Kwa maana mambo yote ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani izidishwe, na Mungu atukuzwe.

Wimbo  wa KAtikati. Zab 126

1. Bwana alipowarejeza mateka wa Sayuni,
    Tulikuwa kama waotao ndoto.
    Ndipo kinywa chetu kilipojaa kicheko,
    Na ulimi wetu kelele za furaha.

(K) Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.

2.   Ndipo waliposema katika mataifa,
Bwana amewatendea mambo makuu.
Bwana ametutendea mambo makuu,
Tulikuwa tukifurahi. (K)

3. Ee Bwana, uwarejeze watu wetu waliofungwa, Kama vijito vya kusini. Wapandao kwa machozi Watavuna kwa kelele za furaha. (K)

4. Ingawa mtu anakwenda zake akilia,
    Azichukuapo mbegu za kupanda.
    Hakika atarudi kwa kelele za furaha,
    Aichukuapo miganda yake. (K)

Injili. Mt 20:20-28

Mama yao wana wa Zebedayo alimwendea Yesu pamoja na wanawe, akamsujudia,na kumwomba neno. Akamwambia,” Wataka nini?” akamwambia, “Agiza kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika ufalme wako.” Yesu akajibu akasema, “Hamjui mnaloliomba. Je! mwaweza kunywea kikombe nitakachonywea mimi?” Wakamwambia, “Twaweza.” Akawaambia, “Hakika mtakinywea kikombe changu; lakini kuketi mkono wangu wa kuume na mkono wangu wa kushoto, sina amri kuwapa, bali watapewa waliowekewa tayari na Baba yangu.” Na wale kumi waliposikia, waliwakasirikia wale ndugu wawili. Lakini Yesu akawaita, akasema “Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”

TAFAKARI.

TUIKARIBISHE NEEMA YA MUNGU: Tunaadhimisha sikukuu ya mtakatifu Yakobo Mkuu. Ndiye mmoja wa wana wa Zebedayo. Alikuwa tayari kuacha aliyoyazoea awali kama mvuvi na kufuatana na Kristo akajifunza kwake na baadaye akatumwa na kuendeleza kazi ya Kristo. Yakobo alijitoa kikamilifu kutetea aliyojifunza kwa Kristo na kuyafundisha hadi kufa shahidi. Ndiye wa kwanza kufa shahidi kati ya wale mitume kumi na wawili. Tunajifunza kwa Mtakatifu Yakobo mambo mengi kama Katekisimu ya Kanisa Katoliki inavyofundisha “Wabatizwa wote wanashiriki katika maisha ya kimungu katika Utatu Mtakatifu neema ya Utakaso, neema ambayo inatufanya kuwa wana wa Mungu na wa Kanisa (KKK 263).” Neema za Mungu ni nyingi kwetu, hata tunapopata shida na changamoto mbalimbali. Tuiruhusu neema ya Mungu kufanya kazi ndani mwetu. Neema hiyo ipate mahali pa kustawi na kukomaa ndani mwetu, tuwe imara tunapokutana na majaribu au changamoto zozote zile na tupate taji la ushindi kama Mtakatifu Yakobo Mtume. 

Sala: Mtakatifu Yakobo mtume utuombee nasi tupate kuishuhudia Imani kwa maneno na matendo yetu.

Masomo ya Misa Julai 24

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 24/07/2024

2024 JULAI 24: JUMATANO-JUMA  LA 16 LA MWAKA

Mt. Sharbel Makhluf
Rangi: Nyeupe

Zaburi: Juma 4

Somo 1. Yer 1: 1, 4-10

Maneno ya Yeremia, mwana wa Hilkia, mmoja wa makuhani waliokuwa katika Anathothi, katika nchi ya Benyamini. Neno la Bwana lilinijia, kusema, kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa.” Ndipo niliposema, “Aa, Bwana Mungu! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.” Lakini Bwana akaniambia, “Usiseme, ‘Mimi ni mtoto;’maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao; maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe. Asema Bwana.Ndipo Bwana akaunyosha mkono wake, akanigusa kinywa changu; Bwana akaniambia, “Tazama, nimetia maneno yangu kinywani mwako; angalia, nimekuweka leo juu ya mataifa na juu ya falme, ili kung’oa, na kubomoa, na kuharibu, na kuangamiza; ili kujenga na kupanda.”

Wimbo wa Katikati. Zab 71: 1-6, 15, 17

1. Nimekukimbilia wewe, Bwana,
Nisiaibike milele.
Kwa haki yako uniponye, uniopoe,
Unitegee sikio lako, uniokoe.

(K) Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako.

2. Uwe kwangu mwamba wa makazi yangu,
Nitakakokwenda siku zote.
Umeamuru niokolewe,
Ndiwe genge langu na ngome yangu.
Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi,
Katika mkono wake mwovu, mdhalimu. (K)

3. Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana Mungu,
Tumaini langu tokea ujana wangu.
Nimekutegemea wewe tangu kuzaliwa,
Ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu,
Ninakusifu wewe daima. (K)

4. Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako.
Mchana kutwa; maana sijui hesabu yake.
Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu;
Nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata leo. (K)

Injili. Mt 13:1-9

Yesu alitoka nyumbani, akaketi kando ya bahari. Wakamkusanyikia makutano mengi, hata akapanda chomboni, akaketi; na ule mkutano wote wakasimama pwani. Akawaambia mambo mengi kwa mifano, akisema,” Tazama, mpanzi alitoka kwenda kupanda. Hata alipokuwa akipanda, mbegu nyingine zilianguka karibu na njia, ndege wakaja wakazila; nyingine zikaanguka penye miamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara zikaota, kwa udongo kukosa kina; na jua lilipozuka ziliungua; na kwa kuwa hazina mizizi zikanyauka. Nyingine zikaanguka penye miiba; ile miiba ikamea, ikazisonga. Nyingine zikaanguka penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia, moja sitini, moja thelathini. Mwenye masikio na asikie.”

TAFAKARI.

TUSHIRIKIANE NA MPANGO WA MUNGU: Uelewa wa tangu zamani ni kuwa, Mungu anamtuma kila mtu ulimwenguni akiwa na ujumbe maalum, akiwa na wimbo maalumu wa kuwaimbia wengine, na akiwa na tendo maalumu la upendo la kufikisha kwa jamii. Hakuna yeyote atakaeupeleka ujumbe wangu alionipa Mungu kwa watu ila mimi mwenyewe. Hakuna yeyote aliye mdogo au mdhaifu, au mzee sana kwamba hawezi kuufikisha ujumbe huo kwa wengine. Kila mmoja wetu atambue, kuna utume wakutimiza hapa duniani. Nabii Yeremia alivyotumwa na Mungu hakuyaelewa haya anajitetea kuwa yeye ni mtoto tu. Mungu anamwambia usiseme kuwa wewe ni mtoto, maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao; maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe. Ndivyo pia kila mwanadamu anayepaswa kusimamia, kutenda na kupeleka wema kwa wengine anapaswa kutiwa moyo kwa maneno hayo. Usijifikirie upo mwenyewe au unafanya kwa nguvu zako mwenyewe bali Mungu ndiye anayetuwezesha. 

Sala: Ee Bwana tuwezeshe kuutambua mpango wako na kushirikiana nawe. Amina.

Masomo ya Misa Julai 23

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 23/07/2024

2024 JULAI 23: JUMANNE-JUMA  LA 16 LA MWAKA

Mt. Birgita, Mtawa
Rangi: Nyeupe

Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mik 7:14-15, 18-20

Walishe watu wako kwa fimbo yako, kundi la urithi wako, wakaao peke yao, mwituni katikati ya Karmeli; na walishe katika Bashani na Gileadi, kama siku za kale. Kama katika siku zile za kutoka kwako katika nchi ya Misri nitamwonyesha mambo ya ajabu. Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema. Atarejea na kutuhurumia; atayakanyaga maovu yetu; nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari. Wewe utamtimizia Yakobo kweli yako, na Ibrahimu rehema zako, ulizowaapia baba zetu tangu siku za kale.

Wimbo wa Katikati. Zab 85:2-8

1. Bwana, umeiridhia nchi yako,
Umewarejeza mateka wa Yakobo.
Umeusamehe uovu watu wako,
Umezisitiri hatia zao zote.
Umeiondoa ghadhabu yako yote,
Umerudi na kuuacha ukali wa hasira yako.

(K) Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako.

2. Mungu wa wokovu wetu, uturudishe,
Uikomeshe hasira uliyo nayo juu yetu.
Je, utatufanyia hasira hata milele?
Utadumisha ghadhabu kizazi hata kizazi? (K)

3. Je, hutaki kurudi na kutuhuisha,
Watu wako wakafurahie?
Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako,
Utupe wokovu wako. (K)

Injili. Mt 12:46-50

Yesu alipokuwa katika kusema na makutano, tazama, mama yake na ndugu zake walikuwa wakisimama nje wataka kusema naye. Mtu mmoja akamwambia,”Tazama, mama yako na ndugu zako wamesimama nje, wanataka kusema nawe.”Akajibu, akamwambia yule aliyempasha habari, “Mama yangu ni nani? Na ndugu zangu ni akina nani?”Akawanyoshea mkono wanafunzi wake, akasema, “Tazama, Mama yangu na ndugu zangu! Kwa maana yeyote atakayeyafanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.”

TAFAKARI.

MAMA NA NDUGU ZAKE KRISTO: Fikiria ukiwa na kaka au dada maarufu, bila shaka hutachoka kumshukuru Mungu kwa ajili yake. Usingechoka watu kukuuliza habari zake huyo unayempenda. Unakuwa na uhakika wa upendeleo wa kuwafikia wapendwa wako kila wakati wa maisha yako. Sehemu ya Injili ya leo, Yesu anatuambia anayeyafanya mapenzi ya Baba yake aliye Mbinguni anafurahia kuwa karibu zaidi nami kuliko ndugu wa damu moja wa kuzaliwa. Hapa Kristo anatupatia maana mpya ya wale wanaoyapokea na kuyafanya mapenzi ya Mungu. Kwa maelezo hayo Kristo hayapunguzii uzito mahusiano ya kindugu wa damu bali anayaboresha yakijumuisha kuyafanya mapenzi ya Mungu. Yeyote anayempokea Mungu kama Bwana na Mchungaji wake, atamsikiliza na kumgeukia katika hali zote za maisha. Ni muhimu kuendelea kumsikiliza na kumgeukia nyakati zote za maisha yetu. Tumsikilize kama kaka yetu, ndiye Mwana wa Mungu aliye hai na Masiha wetu. Anatufundisha mengi sana kama vile kuwa watu wa huruma, kuishi kwa upendo na kusamehe ilivyosisitizwa katika somo la kwanza.  

Sala: Ee Bwana neema yako iendelee kutuwezesha kuyatimiza mapenzi ya Mungu siku zote. Amina.