Select Page

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 06/05/2024

2024 MEI 6 : JUMAMOSI-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Evodi, Askofu
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 2

Mtakatifu Evodi wa Antiokia

by Claretian Publications

Somo 1. Mdo 16:11-15

Tuling’oa nanga kutoka Troa, tukafika Samothrake kwa tanga moja, na siku ya pili tukafika Neapoli; na kutoka hapo tukafika Filipi, mji wa Makedonia, mji ulio mkuu katika jimbo lile, mahali walipohamia Warumi; tukawa katika mji huu, tukikaa siku kadha wa kadha. Hata siku ya Sabato tukatoka nje ya lango, tukaenda kando ya mto, ambapo tukadhani ya kuwa pana mahali pa kusali; tukaketi, tukasema na wanawake waliokutana pale. Mwanamke mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya zambarau, mwenyeji wa Thiatira, mcha Mungu, akatusikiliza, ambaye moyo wake ulifunguliwa na Bwana, ayatunze maneno yaliyonenwa na Paulo. Hata alipokwisha kubatizwa, yeye na nyumba yake, akatusihi, akisema, kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana, ingieni nyumbani mwangu mkakae. Akatushurutisha. 
(K) Bwana awaridhia watu wake.

Wimbo wa Katikati. Zab 149:16, 9

1. Aleluya.
Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Sifa zake katika kusanyiko la watauwa.
Israeli na amfurahie Yeye aliyemfanya,
Wana wa Sayuni na wamshangilie mfalme wao. (K)

2. Na walisifu jina lake kwa kucheza,
Kwa matari na kinubi wamwimbie.
Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake,
Huwapamba wenye upole kwa wokovu. (K)

3. Watauwa na waushangilie utukufu,
Waimbe kwa sauti kuu vitandani mwao.
Sifa kuu za Mungu na ziwe vinywani mwao,
Hiyo ndiyo heshima ya watauwa wote. (K)

Injili. Yn 15:26-16:4

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia. Nanyi pia mnashuhudia, kwa kuwa tangu mwanzo mmekuwapo pamoja nami. Maneno hayo nimewaambia, msije mkachukizwa.  Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada. Na hayo watawatenda kwa sababu hawakumjua Baba wala mimi.  Lakini nimewaambia hayo, ili makusudi saa ile itakapokuja myakumbuke ya kuwa mimi naliwaambia.

TAFAKARI

MAISHA YETU YAMSHUHUDIE KRISTO: Leo katika Injili Yesu anatuahidia Roho Mtakatifu ambaye atamshuhudia. Anatoa mwaliko kwetu sisi tuliobatizwa na kukaa pamoja na Kristo kwa muda mrefu tumshuhudie pia. Maisha ya ushuhuda ni maisha yanayodai sadaka kubwa hata ikibidi kumwaga damu. Yesu anatupa moyo kuwa tusiogope kuishi maisha ya ushuhuda. Kwa kuwa mwaminifu kwa Yesu tunaweza kutengwa na jamii hata kuuawa kama ilivyokuwa kwa Kristo mwenyewe. Tukumbuke kuwa kwa Sakramenti ya Kipaimara tunafanywa kuwa askari hodari wa Yesu Kristo. Tusiache ujumbe wa Kristo upotoshwe kwa sababu ya hofu. Yesu ametuandaa vizuri hivyo tuwe tayari kushuhudia Habari Njema hata kama itatugarimu damu na jasho letu. Tupo katika ulimwengu ambao hauna taswira sahihi ya Mungu, ndiyo maana mambo yanayomhusu Mungu hayapewi kipaumbele. Sisi tuliofunuliwa hayo yote hatuna budi kushuhudia taswira sahihi ya Mungu hata kama ulimwengu utatuchukia.

SALA: Ee Yesu naomba unijalie ujasiri wa kushuhudia imani yangu wakati wote.