Select Page

Masomo ya Misa Aprili 27

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 27/04/2024

2024 APRILI 27 : JUMAMOSI-JUMA LA NNE LA PASAKA

Mt. Zita, Bikira
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 13:44-52

Paulo na wenziwe waliingia katika sinagogi siku ya sabato, wakaketi. Watu wengi, karibu mji wote, wakakusanyika walisikie neno la Mungu. Bali Wayahudi walipowaona makutano, wakajaa wivu, wakayakanusha maneno yaliyonenwa na Paulo, wakibisha na kutukana. Paulo na Barnaba wakanena kwa ushujaa wakasema, Ilikuwa lazima neno la Mungu linenwe kwenu kwanza; lakini kwa kuwa mnalisukumia mbali, na kujiona nafsi zenu kuwa hamkustahili uzima wa milele, angalieni, twawageukia Mataifa. Kwa sababu ndivyo tulivyoamriwa na Bwana, Nimekuweka uwe nuru ya Mataifa, upate kuwa wokovu hata mwisho wa dunia. Mataifa waliposikia hayo wakafurahi, wakalitukuza neno la Bwana, nao waliokuwa wamekusudiwa uzima wa milele wakaamini. Neno la Bwana likaenea katika nchi ile yote. Lakini Wayahudi wakawafitinisha wanawake watauwa wenye cheo na wakuu wa mji, wakawataharakisha watu wawaudhi Paulo na Barnaba; wakawatoa katika mipaka yao. Nao wakawakung’utia mavumbi ya miguu yao, wakaenda Ikonio. Na wanafunzi walijaa furaha na Roho Mtakatifu.

Wimbo wa Katikati. Zab 98:1-4

“1. Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Kwa maana ametenda mambo ya ajabu.
Mkono wa kuume wake mwenyewe,
Mkono wake mtakatifu umemtendea wokovu. (K)

2. Machoni pa mataifaameidhihirisha haki yake.
Amezikumbuka rehema zake,
Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli. (K)

3. Miisho yote ya dunia imeuona
Wokovu wa Mungu wetu.
Mshangilieni Bwana, nchi yote,
Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi. (K) “

(K) Miisho yote ya dunia imeuona Wokovu wa Mungu wetu.

Injili. Yn 14:7-14

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba, tangu sasa mnamjua, tena mmemwona. Filipo akamwambia, Bwana, utuonyeshe Baba, yatutosha. Yesu akamwambia, Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe wasemaje, Utuonyeshe Baba? Husadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu? Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake. Mnisadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu; la! hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe. Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba. Nanyi mkiomba lo lote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana. Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya.

SALA: Ee Kristo utujalie tutende kadiri ya mapenzi yako.

TAFAKARI

TUKIMWAMINI KRISTO TUTATENDA: Tunamaliza wiki ya nne ya Pasaka kwa ujumbe mzito kwa maneno ya Kristo akitualika kuomba kwa jina lake. Ni ujumbe kutoka injili ya leo (Yoh. 14:7-14). Yesu anamwelekeza Filipo namna ya kumwona Baba. Kwamba aliyemwona Mwana amemwona Baba. Lakini msisitizo mkuu unawekwa ktk kuamini, kwani anayemwamini Kristu anaweza kufanya makuu. Tukiwa na imani tunahakikishiwa kupata lolote tuombalo. Na hasa kama hilo tuombalo tunaliomba kwa jina la Yesu kwa njia ya sala zetu. Yesu ananiambia mimi, anakuambia wewe na anamwambia kila mmoja wetu: “Mkiomba lolote kwa jina langu, hilo nitalifanya.” Tuchukue nafasi hii wakati huu wa Pasaka kujifunza kuyaweka maneno ya Kristo katika matendo yetu kwa imani na sala. Aidha tujifunze kutoka mitume ambao waliyaweka matendo na maneno yao yote katika sala wakimtanguliza Mungu awajalie kile walichomwomba kwani Yes anasema “Yeye aniaminiye mimi, kazi nifanyazo mimi, yeye naye atazifanya.”

Masomo ya Misa Aprili 26

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 26/04/2024

2024 APRILI 26 : IJUMAA-JUMA LA NNE LA PASAKA

Mt. Kleti, Papa na Mfiadini
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 13:26-33

Paulo alisimama akawapungia mkono, akasema: ndugu zangu, wana wa ukoo wa Ibrahimu, na hao miongoni mwenu wanaomcha Mungu, kwetu sisi neno la wokovu huu limepelekwa. Kwa maana wakaao Yerusalemu, na wakuu wao, kwa kuwa hawakumjua yeye, wala maneno ya manabii yanayosomwa kila Sabato, wameyatimiza kwa kumhukumu. Na ijapokuwa hawakuona sababu ya kumfisha wakamwomba Pilato auawe. Hata alipokwisha kumaliza yote aliyoandikiwa, wakamtelemsha katika ule mti, wakamweka kaburini. Lakini Mungu akamfufua katika wafu; akaonekana siku nyingi na wale waliopanda naye kutoka Galilaya hata Yerusalemu, ambao sasa ndio walio mashahidi wake mbele ya watu. Na sisi tunawahubiri Habari Njema ya ahadi ile waliyopewa mababa, ya kwamba Mungu amewatimizia watoto wetu ahadi hiyo, kwa kumfufua Yesu kama ilivyoandikwa katika zaburi ya pili, Wewe ndiwe Mwanangu, mimi leo nimekuzaa.

Wimbo wa Katikati. Zab 2:6-11

“1. Nami nimemweka mfalme wangu
Juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu
Nitaihubiri amri; Bwana aliniambia
Ndiwe mwanangu, mimi leo nimekuzaa. (K)

K) Ndiwe mwanangu, Mimi leo nimekuza

2. Uniombe, nami nitakupa mataifa kuwa urithi wako,
Na miisho ya dunia kuwa milki yako.
Utawaponda kwa fimbo ya chuma,
Na kuwavunja kama chombo cha mfinyanzi. (K)

3. Na sasa, enyi wafalme, fanyeni akili,
Enyi waamuzi wa dunia, mwadibiwe.
Mtumikieni Bwana kwa kicho,
Shangilieni kwa kutetemeka. (K)

Injili. Yn 14:1-6

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia, maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi muwepo. Nami niendako mwaijua njia. Tomaso akamwambia, Bwana, sisi hatujui uendako; nasi twaijuaje njia? Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.

TAFAKARI

YESU NI NJIA YETU HALISI: Padre mmoja mgeni alipotea njia. Akawaambia watoto “Nionesheni njia ya kwenda parokiani, nami niwaoneshe njia ya kwenda mbinguni.” Mtoto mmoja akamjibu “Wewe hujui njia ya kwenda parokiani utawezaje kuijua njia ya kwenda mbinguni?” Yesu akiwa njia maana yake ni kwamba ili kufika mbinguni hatuna budi kumfuata Yeye. Amfuataye Yesu hapotei bali hufika anakoelekea, mbinguni. Tukimfuata Yesu hatuhitaji kumuuliza mtu yeyote tunakoelekea. Lengo la kumfuata Yesu aliye njia ni ili atujulishe ukweli kwani Yeye ndiye kweli halisi. Walimu hufundisha ukweli wakati wao sio ukweli. Lakini Yesu si tu kwamba hufundisha ukweli bali Yeye ni kweli yenyewe. Yesu ni njia ielekezayo kwenye uzima. Je, wataka kufika kwa Baba? Usitafute njia kwani Yesu ni njia. Je, wataka kujifunza na kuujua ukweli, Yesu ndiye kweli yenyewe. Je, wataka kuupata uzima? Ukimpata Yesu umeupata uzima. Wakati huu wa Pasaka hatuna budi kusikia sauti ya Yesu asemaye “Mimi ndimi njia, na kweli na uzima. Mtu haji kwa Baba ila kwa njia ya mimi”(Yoh 14:6).

SALA: Ee Yesu uliye njia yetu halisi, utujalie tukufuate wewe daima.

Masomo ya Misa Aprili 25

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 25/04/2024

2024 APRILI 25 : ALHAMISI-JUMA LA NNE LA PASAKA

MT. MARKO, MWINJILI
Rangi: Nyekundu
Zaburi: Juma 4

Somo 1. 1Pet 5:5-14

Ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu. Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani. Na Mungu wa neema yote, aliyewaita kuingia katika utukufu wake wa milele katika Kristo, mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu. Uweza una yeye hata milele na milele. Amina. Kwa mkono wa Silwano, ndugu mwaminifu kama nionavyo, nimewaandikia kwa maneno machache, kuonya na kushuhudia ya kuwa hii ndiyo neema ya kweli ya Mungu. Simameni imara katika hiyo. Mwenzenu mteule hapa Babeli awasalimu, na Marko mwanangu. Salimianeni kwa busu la upendo. Amani na iwe kwenu nyote, mlio katika Kristo. Amina.

(K). Fadhili zako nitaziimba milele, Ee Bwana. 

Wimbo wa Katikati. Zab 89:2-3, 6-7, 16 -17

“1. Fadhili za Bwana nitaziimba milele;
Kwa kinywa changu nitavijulisha vizazi vyote uaminifu wako.
Maana nimesema, Fadhili zitajengwa milele;
Katika mbingu utauthibitisha uaminifu wako. (K)

2. Ee Bwana, mbingu zitayasifu maajabu yako,
Uaminifu wako katika kusanyiko la watakatifu.
Maani ni nani katika mbingu awezaye kulinganishwa na Bwana?
Ni nani afananaye na Bwana miongoni mwa alaika? (K)

3. Heri watu wale waijuao sauti ya shangwe,
Ee Bwana, huenenda katika nuru ya uso wako.
Kwa jina lako hufurahi mchana kutwa,
Na kwa haki yako hutukuzwa. (K)”

Injili. Mk 16:15-20

Yesu aliwaambia wale Kumi na mmoja, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya. Basi Bwana Yesu, baada ya kusema nao, akachukuliwa juu mbinguni, akaketi mkono wa kuume wa Mungu. Nao wale wakatoka, wakahubiri kotekote, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo.

TAFAKARI

TUMEBATIZWA NA TUMETUMWA: Leo Kanisa linasherehekea sikukuu ya Marko Mwinjili. Tunaelezwa kuwa huyu aliandamana sana na Barnabas, Paulo na Petro na hata Injili aliyoandika imegusia kwa kiasi kikubwa mafundisho ya Petro. Alichangia kwa kiasi kikubwa kukuza imani ya Waamini wa Kanisa la mwanzo hasa barani Afrika. Alivaa moyo wa unyenyekevu kama somo la kwanza lilivyotuambia, ambao ulimfanya kuwa tayari kujisadaka, aliweza kumpinga adui wa imani yetu kwa kuwa imara na thabiti katika imani. Kwa kufanya hivi alitimiza hili analosema Yesu katika Injili, “enendeni ulimwenguni mwote mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe.” Kristo anatualika nasi leo hii tuendeleze utume huu wa kuitangaza Injili yake kwa watu wote. Ziko namna nyingi za kutangaza Injili kama kujitolea kwa ajili ya ujenzi wa makanisa, kusali, kusoma na kutafakari Neno la Mungu, kujiunga katika vyama vya kitume, kuishi maisha maadili, kutoa malezi kwa watoto na vijana, n.k.

SALA: Ee Mungu utupe neema ya kuwa wamisionari wa Neno lako.

Masomo ya Misa Aprili 24

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 24/04/2024

2024 APRILI 24 : JUMATATU-JUMA LA NNE LA PASAKA

Mt. Fideli wa Stigmaringen, Padre na Shahidi
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 12:24, 13:5

Siku zile, neno la Bwana likazidi na kuenea. Na Barnaba na Sauli, walipokwisha kutimiza huduma yao, wakarejea kutoka Yerusalemu, wakamchukua pamoja nao Yohane aitwaye Marko. Na huko Antiokia katika Kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao. Basi watu hao, wakiisha kupelekwa na Roho Mtakatifu wakatelemkia Seleukia, na kutoka huko wakasafiri baharini hata Kipro. Na walipokuwa katika Salami wakalihubiri neno la Mungu katika masinagogi ya Mayahudi.

Wimbo wa Katikati. Zab 67:2-3, 5-6, 8

“1. Mungu na atufadhili na kutubariki,
Na kutuangazia uso wake.
Njia yake ijulike duniani,
Wokovu wake katikati ya mataifa yote. (K)

2. Mataifa na washangilie,
Naam, waimbe kwa furaha,
Maana kwa haki utawahukumu watu,
Na kuwaongoza mataifa walioko duniani. (K)

3. Watu na wakushukuru, Ee Mungu,
Watu wote na wakushukuru.
Mungu atatubariki sisi;
Miisho yote ya dunia itamcha Yeye. (K) “

(K) Watu na wakushukuru, Ee Mungu, Watu wote na wakushukuru.  

Injili. Yn 12:44-50

Siku ile Yesu alipaza sauti, Yeye aniaminiye mimi, haniamini mimi bali yeye aliyenipeleka. Naye anitazamaye mimi amtazama yeye aliyenipeleka. Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani. Na mtu akiyasikia maneno yangu, asiyashike, mimi simhukumu; maana sikuja ili niuhukumu ulimwengu, ila niuokoe ulimwengu. Yeye anikataaye mimi, asiyeyakubali maneno yangu, anaye amhukumuye; neno hilo nililolinena ndilo litakalomhukumu siku ya mwisho. Kwa sababu mimi sikunena kwa nafsi yangu tu; bali Baba aliyenipeleka, yeye mwenyewe ameniagiza nitakayonena na nitakayosema. Nami najua ya kuwa agizo lake ni uzima wa milele; basi hayo ninenayo mimi, kama Baba alivyoniambia, ndivyo ninenavyo.

SALA: Tunakuomba ewe Roho Mtakatifu utuwezeshe kuwa wasikivu kwa Kristo.

TAFAKARI

KAZI YA MUNGU LAZIMA ITENDEKE: Yesu anatualika tumsikie yeye na tutekeleze yale anayotuambia vinginevyo hali yetu mbeleni hatutabaki salama. Anataka kila mmoja wetu kazi ambayo kwayo Mungu alimuumba aitekeleze. Anatueleza kuwa maneno aliyotuambia ni kutoka kwa Baba yake na sio yake. Maneno haya ndiyo yaliyowapa nguvu mitume kokote walikotawanyikia, (rej. somo 1), “siku zile Neno la Bwana likazidi na kuenea…na Barnaba na Sauli wakatengwa kwa kazi ile waliyoitiwa.” Hapa tunaona jinsi mitume walivyohangaika kuhakikisha kuwa utume wa Kanisa unaendelea. Mtume Paulo anaeleza tabia za mtu anayeendeleza kazi hii ya kusambaza Neno la Mungu kwamba “awe mtu asiyeshtakiwa kwa neno, asijipendekeze, asitafute maslahi binafsi, asipende mapato ya aibu, awe mkaribishaji, mpenda mema, mwenye kiasi…” (Tit 1:7-9). Hivi ni vielelezo vya kumsaidia mtu katika utume na anajikuta anautekeleza vyema, na hii itamsaidia kuwa msikivu kwa sauti ya Kristo anayetuhabarisha habari toka kwa Baba yake wa mbinguni.

 

Masomo ya Misa Aprili 23

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 23/04/2024

2024 APRILI 23 : JUMATATU-JUMA LA NNE LA PASAKA

Mt. Georgi, Shahidi
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 11:19-26

Siku zile, wale waliotawanyika kwa sababu ya ile dhiki iliyotukia kwa habari ya Stefano, wakasafiri hata Foinike na Kipro na Antiokia, wasilihubiri lile neno ila kwa Wayahudi peke yao. Lakini baadhi ya hao walikuwa watu wa Kipro na Kirene, nao walipofika Antiokia wakasema na Wayahudi wa Kiyunani, wakihubiri Habari Njema za Bwana Yesu. Mkono wa Bwana ukawa pamoja nao; watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana. Habari hizo za watu hao zikafika masikioni mwa Kanisa lililokuwako katika Yerusalemu; wakamtuma Barnaba, aende hata Antiokia. Naye, alipokwisha kufika na kuiona neema ya Mungu akafurahi, akawasihi wote waambatane na Bwana kwa kusudi la moyo. Maana alikuwa mtu mwema amejaa Roho Mtakatifu na imani; watu wengi wakaongezeka upande wa Bwana. Kisha akatoka akaenda Tarso kumtafuta Sauli; hata alipokwisha kumwona akamleta Antiokia. Ikawa kwa muda wa mwaka mzima wakakusanyika pamoja na Kanisa na kuwafundisha watu wengi. Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza hapo Antiokia.

(K) Enyi mataifa yote, msifuni Bwana.

Wimbo wa Katikati. Zab 87:1-7

“1. Msingi wake upo
Juu ya milima mitakatifu.
Bwana ayapenda malango ya Sayuni
Kuliko maskani zote za Yakobo.
Umetajwa kwa mambo matukufu,
Ee Mji wa Mungu. (K)

2. Nitataja Rahabu na Babeli
Miongoni mwao wanaonijua.
Tazama Filisti, na Tiro, na Kushi;
Huyu alizaliwa humo.
Naam, mintarafu Sayuni itasemwa,
Huyu na huyu walizaliwa humo. (K)

3. Na Yeye Aliye juu
Ataufanya imara.
Bwana atahesabu, awaandikiapo mataifa,
Huyu alizaliwa humo.
Waimbao na wachezao na waseme,
Visima vyangu vyote vimo mwako. (K)”

Injili. Yn 10: 22-30

Huko Yerusalemu ilikuwa Sikukuu ya Kutabaruku; ni wakati wa baridi. Naye Yesu alikuwa akitembea hekaluni, katika ukumbi wa Sulemani. Basi Wayahudi walimzunguka, wakamwambia, Hata lini utatuhangaisha nafsi zetu? Kama wewe ndiwe Kristo, utuambie waziwazi. Yesu akawajibu, Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia. Lakini ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu. Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu. Mimi na Baba tu umoja.

TAFAKARI

Huko Yerusalemu ilikuwa Sikukuu ya Kutabaruku; ni wakati wa baridi. Naye Yesu alikuwa akitembea hekaluni, katika ukumbi wa Sulemani. Basi Wayahudi walimzunguka, wakamwambia, Hata lini utatuhangaisha nafsi zetu? Kama wewe ndiwe Kristo, utuambie waziwazi. Yesu akawajibu, Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia. Lakini ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu. Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu. Mimi na Baba tu umoja.

 

Masomo ya Misa Aprili 22

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 22/04/2024

2024 APRILI 22 : JUMATATU-JUMA LA NNE LA PASAKA

Mt. Konrad wa Parzam, Mtawa Mfransisko
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 11:1-18

Siku zile, mitume na ndugu waliokuwako katika Uyahudi wakapata habari ya kwamba watu wa Mataifa nao wamelipokea neno la Mungu. Na Petro alipopanda kwenda Yerusalemu, wale walio wa tohara wakashindana naye, wakisema, Uliingia kwa watu wasiotahiriwa ukala nao. Petro akaanza kuwaeleza kwa taratibu, akasema, Nalikuwa katika mji wa Yafa, nikiomba, roho yangu ikazimia, nikaona maono; chombo kinashuka, kama nguo kubwa inatelemshwa kutoka mbinguni kwa pembe zake nne, kikanifikia. Nikakitazama sana, nikifikiri, nikaona wanyama wa nchi wenye miguu minne, na wanyama wa mwituni, nao watambaao, na ndege wa angani. Nikasikia na sauti ikiniambia, Ondoka; Petro, ukachinje ule. Nikasema, Hasha, Bwana, kwa maana kitu kilicho kichafu au kilicho najisi hakijaingia kabisa kinywani mwangu. Sauti ikanijibu mara ya pili kutoka mbinguni, alivyovitakasa Mungu, usivinene wewe najisi. Jambo hili likatendeka mara tatu, kisha vitu vyote vikavutwa tena juu mbinguni. Na tazama, mara hiyo watu watatu wakasimama mbele ya nyumba tuliyokuwamo waliotumwa kwangu kutoka Kaisaria. Roho akaniambia nifuatane nao, nisione tashwishi. Ndugu hawa sita nao wakaenda nami, tukaingia katika nyumba ya mtu yule; akatueleza jinsi alivyomwona malaika aliyesimama nyumbani mwake na kumwambia, tuma watu kwenda Yafa ukamwite Simoni aitwaye Petro, atakayekuambia maneno ambayo yatakuokoa, wewe na nyumba yako yote. Ikawa nilipoanza kunena, Roho Mtakatifu akawashukia kama alivyotushukia sisi mwanzo. Nikalikumbuka neno lile la Bwana, jinsi alivyosema, Yohane alibatiza kwa maji kweli, bali ninyi mtabatiza kwa Roho Mtakatifu. Basi, ikiwa Mwenyezi Mungu amewapa wao karama ile ile aliyotupa sisi tuliomwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani niweze kumpinga Mungu? Waliposikia maneno haya wakanyamaza, wakamtukuza Mungu, wakisema, Basi, Mungu amewajalia hata mataifa nao toba liletalo uzima.

Wimbo wa Katikati. Zab 42:2-3.43:3-4

“1. Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji,
Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, ee Mungu. (K)

2. Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai,
Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu? (K)

3. Nilitewe nuru yako na kweli yako ziniongoze,
zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu na hata maskani yako. (K)

4. Hivyo nitakwenda madhabahuni kwa Mungu,
kwa Mungu aliye furaha yangu na shangwe yangu;
Nitakusifu kwa kinubi, ee Mungu, Mungu wangu. (K)”

K) Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai.  
K) Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai.  

Injili. Yn 10: 1-10

Yesu alisema: Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo. Mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwamwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia; na mbwamwitu huwakamata na kuwatawanya. Yule hukimbia kwa kuwa ni mtu wa mshahara; wala mambo ya kondoo si kitu kwake. Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo. Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja. Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.

TAFAKARI

YESU NI MCHUNGAJI WETU: Kanisa Katoliki limekabidhiwa jukumu la kuwaelekeza watu wote kumjua Mungu. Katekisimu ya Kanisa Katoliki inasema, “Sakramenti ya ubatizo ndiyo inayomwondolea mtu dhambi ya Asili pamoja na dhambi nyinginezo, kutupatia neema ya utakaso, kutuandika watoto wa Mungu na wa Kanisa.” Ni kwa sakramenti hii tunaanza safari ya kuwa kondoo na tunapaswa kuwa chini ya mchungaji wetu Yesu Kristo. Kanisa linapaswa kuelewa kuwa, lina wajibu si tu wa kuwalinda walio ndani bali hata kuwatafuta na kuwarudisha waliopotea, (walegevu). Ukiangalia mfumo tulionao sasa wa Jumuiya Ndogondogo za Kikirsto utagundua kwa urahisi sana ni wapi kuna shida katika kuiishi imani yetu. Haitoshi kusubiri mpaka mtu afe na fomu yake kujazwa kuwa ‘hastahili kufanyiwa maziko ya Kikristo’’ kutokana na namna yake alivyokuwa anaishi. Injili hii inatutaka tumrekebishe kabla na hii ni kazi yetu sote, sio suala la kusema ni kazi ya mapadre/maaskofu la hasha, kila mbatizwa anapaswa kumlinda mwenzake, kuwa mchunguji mwema kama Kristo mwenyewe.

SALA: Ee Mungu utujalie tutambue wajibu wa kuwaongoza walio walegevu kiimani.