Select Page

Masomo ya Misa Mei 6

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 06/05/2024

2024 MEI 6 : JUMAMOSI-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Evodi, Askofu
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 2

Mtakatifu Evodi wa Antiokia

by Claretian Publications

Somo 1. Mdo 16:11-15

Tuling’oa nanga kutoka Troa, tukafika Samothrake kwa tanga moja, na siku ya pili tukafika Neapoli; na kutoka hapo tukafika Filipi, mji wa Makedonia, mji ulio mkuu katika jimbo lile, mahali walipohamia Warumi; tukawa katika mji huu, tukikaa siku kadha wa kadha. Hata siku ya Sabato tukatoka nje ya lango, tukaenda kando ya mto, ambapo tukadhani ya kuwa pana mahali pa kusali; tukaketi, tukasema na wanawake waliokutana pale. Mwanamke mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya zambarau, mwenyeji wa Thiatira, mcha Mungu, akatusikiliza, ambaye moyo wake ulifunguliwa na Bwana, ayatunze maneno yaliyonenwa na Paulo. Hata alipokwisha kubatizwa, yeye na nyumba yake, akatusihi, akisema, kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana, ingieni nyumbani mwangu mkakae. Akatushurutisha. 
(K) Bwana awaridhia watu wake.

Wimbo wa Katikati. Zab 149:16, 9

1. Aleluya.
Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Sifa zake katika kusanyiko la watauwa.
Israeli na amfurahie Yeye aliyemfanya,
Wana wa Sayuni na wamshangilie mfalme wao. (K)

2. Na walisifu jina lake kwa kucheza,
Kwa matari na kinubi wamwimbie.
Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake,
Huwapamba wenye upole kwa wokovu. (K)

3. Watauwa na waushangilie utukufu,
Waimbe kwa sauti kuu vitandani mwao.
Sifa kuu za Mungu na ziwe vinywani mwao,
Hiyo ndiyo heshima ya watauwa wote. (K)

Injili. Yn 15:26-16:4

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia. Nanyi pia mnashuhudia, kwa kuwa tangu mwanzo mmekuwapo pamoja nami. Maneno hayo nimewaambia, msije mkachukizwa.  Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada. Na hayo watawatenda kwa sababu hawakumjua Baba wala mimi.  Lakini nimewaambia hayo, ili makusudi saa ile itakapokuja myakumbuke ya kuwa mimi naliwaambia.

TAFAKARI

MAISHA YETU YAMSHUHUDIE KRISTO: Leo katika Injili Yesu anatuahidia Roho Mtakatifu ambaye atamshuhudia. Anatoa mwaliko kwetu sisi tuliobatizwa na kukaa pamoja na Kristo kwa muda mrefu tumshuhudie pia. Maisha ya ushuhuda ni maisha yanayodai sadaka kubwa hata ikibidi kumwaga damu. Yesu anatupa moyo kuwa tusiogope kuishi maisha ya ushuhuda. Kwa kuwa mwaminifu kwa Yesu tunaweza kutengwa na jamii hata kuuawa kama ilivyokuwa kwa Kristo mwenyewe. Tukumbuke kuwa kwa Sakramenti ya Kipaimara tunafanywa kuwa askari hodari wa Yesu Kristo. Tusiache ujumbe wa Kristo upotoshwe kwa sababu ya hofu. Yesu ametuandaa vizuri hivyo tuwe tayari kushuhudia Habari Njema hata kama itatugarimu damu na jasho letu. Tupo katika ulimwengu ambao hauna taswira sahihi ya Mungu, ndiyo maana mambo yanayomhusu Mungu hayapewi kipaumbele. Sisi tuliofunuliwa hayo yote hatuna budi kushuhudia taswira sahihi ya Mungu hata kama ulimwengu utatuchukia.

SALA: Ee Yesu naomba unijalie ujasiri wa kushuhudia imani yangu wakati wote.

Masomo ya Misa Mei 5

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 05/05/2024

2024 MEI 5 : DOMINIKA YA 6 YA PASAKA

Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 

Somo 1. Mdo 10: 25-26, 34 -35, 44-48

Petro alipokuwa akiingia Kornelio akatoka amlaki akamwangukia miguu, akamsujudia. Lakini Petro akamwinua, akasema, Simama, mimi nami ni mwanadamu. Petro akafumbua kinywa chake, akasema, Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo, bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye. Petro alipokuwa akisema maneno hayo Roho Mtakatifu akawashukia wote waliolisikia lile neno. Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha, na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu, Ni nani awezaye kukataza maji, hawa wasibatizwe, watu waliopokea Roho Mtakatifu vile vile kama sisi? Akaamuru wabatizwe kwa jina lake Yesu Kristo. Ndipo wakamsihi azidi kukaa siku kadha wa kadha.

Wimbo wa Katikati. Zab 98: 1 – 4

“1. Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Kwa maana ametenda mambo ya ajabu.
Mkono wa kuume wake mwenyewe,
Mkono wake mtakatifu umemtendea wokovu. (K)

2. Bwana ameufunua wokovu wake,
Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake.
Amezikumbuka rehema zake,
Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli. (K)

3. Miisho yote ya dunia imeuona
Wokovu wa Mungu wetu.
Mshangilieni Bwana, nchi yote,
Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi. (K)”

(K) Bwana ameufunua wokovu wake, Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake.

Somo 2. 1 Yoh 4: 7 -10

Wapenzi, na tupendane; kwa kuwa pendo latoka kwa Mungu, na kila apendaye amezaliwa na Mungu, naye anamjua Mungu. Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo. Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.

Injili. Yn 15: 9-17

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Kama vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe. Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi. Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo. Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu. Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni. Haya nawaamuru ninyi, mpate kupendana.

TAFAKARI

“FURAHA YA KWELI INAPATIKANA KATIKA KRISTO
Hati ya kichungaji ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vaticano juu ya Kanisa katika ulimwengu mamboleo «Furaha na Matumaini (Gaudium et Spes) »inasema hivi: “Ukweli ni kwamba katika fumbo la Neno la Mungu kufanyika mwili ndipo fumbo la mwanadamu linafumbuliwa. Hii ni kwa sababu Adam, mwanadamu wa mwanzo kabisa alikuwa taswira ya yeye Kristo Yesu ambaye alipaswa kutujia. Kristo ambaye ni Adam wa mwisho amemfunulia mwanadamu ukweli kuhusu asili yake na ukweli juu ya wito wake mkuu kwa kuufunua upendo wa Baba na upendo wake” (Namba 22). Sehemu hii ya waraka wa Mtaguso inanuia kutuonesha tija ya fumbo la umwilisho ambalo kwalo majawabu mengi kuhusiana na changamoto zinazomkabili mwanadamu hupata majawabu yake. Moja ya changamoto hizo ni furaha. Ni ipi iliyo furaha ya kweli?
Kiuhalisia mwanadamu anatamani kuwa katika hali ya furaha daima lakini je, ni ipi iliyo kwake furaha ya kweli na ya kudumu? Furaha ya kweli inapatikana katika Kristo. Mtakatifu Bernadetha Subiru aliambiwa na Mama Bikira Maria kwamba anamuahidi furaha lakini si katika maisha ya ulimwengu huu bali maisha ya baadaye. Kristo anatuambia katika Injili ya leo: “Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe.” Hivyo mambo mawili yanawekwa wazi kama nyenzo ya kuifikia furaha kamilifu, yaani kuzishika amri za Mungu na kukaa katika pendo la Mungu.
Utimilifu wetu wanadamu unapatikana katika kuungana na Kristo. Dhana hii imetafakariwa kwa kirefu katika Dominika mbili zilizopita ambapo Kristo alijitanabaisha kama Mchungaji wa Kondoo na mzabibu wa kweli. Fumbo la umwilisho kama nilivyodokeza hapo mwanzoni limeweka wazi ukweli kuhusu mwanadamu na ukweli huo unajionesha katika muunganiko kamilifu na Kristo na kwa njia yake na Mungu Baba. Muunganiko huo hutekelezwa kwa njia ya kuzishika amri za Mungu ambazo ndizo miongozo na kanuni za kuipata furaha ya kweli na inayodumu. Hakuna kitu chochote kinachoweza kuwa katika ukamilifu bila kufuata kanuni za kuundwa kwake. Gari likiacha kufuata kanuni za kuundwa kwake matairi yakagoma kwenda au breki zikaacha kukamata sawasawa au taa ya kuashiria kulia au kushoto ikaacha kuwaka matokeo yake ni majanga na uharibifu. Hivi ndivyo kwetu sisi wanadamu. Hatukujiumba au kujileta duniani kwa utashi wetu wenyewe. Tunapoacha kuunganika na Yeye aliyetufanya kwa kuendana na kanuni anazotuwekea tunaingia katika ukengeufu na mwisho ni majanga.
Changamoto tuipatayo katika ulimwengu mamboleo ni kuenea kwa uhuru wa mwanadamu katika kutafuta auheni ya maisha na furaha. Namna hii imetuondoa katika kulitazama neno la Mungu na matokeo yake tunajitafutia namna zetu kadiri ya vionjo vyetu na misukumo ya kibinadamu. Matokeo yake ni dhahiri: ni anguko kwa mwanadamu na udhalilishaji wa utu wa mtu. Uhuru tunaojivika unamithilika na uhuru bandia kwani wengi hujikuta tumeingia katika misukosuko na matatizo mengi badala ya kupata uhuru wa kweli. Kristo ambaye ni ufunuo wa uhuru wa kweli katika kutafuta furaha ya kudumu ametufundisha bustanini Getsemani namna ya kuonesha uhuru wako hali umeunganika na mapenzi ya Mungu, yaani amri zake. Akiwa katika hali ya huzuni kubwa kiasi cha kutokwa na jasho la damu alisali akisema: “Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke” (Lk 22:42). Kama binadamu anatamani kupata faraja na furaha ya kudumu lakini akiwa ameunganika na Baba yake anataka kuipata furaha hiyo kadiri ya mapenzi yake.
Tunapoitafuta furaha bila kuunganika na Mungu tunaishia katika furaha za muda mfupi. Hili kwa namna ya pekee huonekana katika furaha tuitafutayo kwa kuwatumia wenzetu kama vyombo. Ni namna ambavyo mwanadamu anafumba macho na kutoona muunganiko wa asilia uliopo kati yake na ndugu yake pembeni yake na hivyo kumweka mbele yake kama chombo cha kujinufaisha na kuifurahisha nafsi yake. Namna hii kamwe haitupatii furaha ya kweli. Hata tukijidanganya kwa kusema kila mmoja ahangaike na hali yake lakini bado damu yake itakuita tu. Unyonyaji, manyanyaso, mateso na uhasi mwingine dhidi ya mwanadamu mwenzako hukurudia mwenyewe tu. Nahau ya kiingereza isemayo what goes around comes around itugutushe katika hilo.
Ndiyo maana Kristo anaipanua namna ya kuufanya upendo wetu utupatie furaha ya kudumu: “Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi. Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” Furaha yetu ya kweli inaonekana kwanza katika mwelekeo wa upendo kwa Mungu na pili katika mwelekeo wa upendo wetu kwa jirani. Kristo anaendelea kuwa kielelezo kwetu kwa namna hiyo kama anavyofafanua Mtume Yohane katika somo la pili la Dominika hii. Hii namna ya kujitoa nafsi yako, kujisadaka kwa ajili ya wenzako. Sehemu hiyo ya Maandiko matakatifu inapigia mstari dhana ya Mungu kuwa asili au sababu ya yote ayatendayo mwanadamu. Upendo wetu kwa wenzetu asili yake si sisi; asili yake tunapaswa kuiona katika Mungu: “Wapenzi na tupendane; kwa kuwa pendo latoka kwa Mungu, na kila apendaye amezaliwa na Mungu, naye anamjua Mngu.” Hivyo namna yoyote ya upendo kati yetu sisi kwa sisi inapaswa kuchipuka katika Yeye kupitia Kristo Bwana wetu.
Upendo huo ambao unapata asili yake katika Mungu unatutajirisha zaidi kwa kuunganika na watu wote na pia kuona utendaji wa Mungu katika kila kazi njema ya mwanadamu. Petro anapoingia nyumbani kwa Kornelio anatamka kwa ujasiri akisema: “hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo, bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” Petro amefanya tamko hilo baada ya maono aliyoyapata katika aya zilizotangulia somo la leo, aya ambazo zilimfunulia namna utendaji Mungu unavyotenda kazi kwa wanadamu wote. Kristo anayeufunua ubinadamu wetu katika hali yake stahiki anaugusa ubinadamu wote na yeyote anayeifuata njia yake kwa njia ya neema ya Mungu ataweza kumtukuza Mungu na hivyo kuingia katika kundi la wale wanaozishika amri zake na hivyo sote tutaipata furaha ya kweli.
Hivyo tuitikie wito wa Kristo katika hitimisho la Injili ya leo. Yeye anatutaka tuendelee kubaki katika urafiki na Yeye kwa kusikiliza na kuliishi lile analotufundisha. Hali hiyo itatufanya kuwa wana huru na si watumwa. Hii ni kwa sababu kwa kulisikiliza Neno lake tutayafahamu yale anayotuamuru kufanya na yale anayoyatenda lakini “mtumwa hajui atendalo bwana wake.” Ni wito wa kujitajirisha na habari za ufalme wa Mungu kwa kuisikiliza sauti ya Kristo ambaye anatuambia yote anayoyasikia kwa Mungu Baba aliye chanzo na maana ya ubinadamu wetu na pia chimbuko la furaha yetu ya kweli.”

SALA: Ee Kristo Mfufuka utujaze furaha katika upendo wako.

Masomo ya Misa Mei 4

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 04/05/2024

2024 MEI 4 : JUMAMOSI-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Godehardi, Askofu”
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 1

Somo 1. Mdo 16:1-10

Siku zile, Paulo alifika Derbe na Listra na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. Mtu huyo alishuhudiwa vyema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio. Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtairi kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani. Basi walipokuwa wakipita kati ya miji ile wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike. Makanisa yakatiwa nguvu katika ile imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku. Wakapita katika nchi ya Frigia na Galatia, wakikatazwa na Roho Mtakatifu, wasilihubiri lile neno katika Asia. Walipofika kukabili Misia, wakajaribu kwenda Bithinia, lakini Roho wa Yesu hakuwapa ruhusa, wakapita Misia wakatelemka Troa. Paulo akatokewa na maono usiku; alimwona mtu wa Makedonia amesimama, akimsihi, na kumwambia, vuka, uje Makedonia utusaidie. Basi alipokwisha kuyaona yale maono, mara tukataka kutoka kwenda Makedonia, kwa kuwa tuliona hakika ya kwamba Mungu ametuita tuwahubiri Habari Njema.

Wimbo wa Katikati. Zab 100:1-3, 5

“1. Mfanyieni Bwana shangwe, dunia yote
Mtumikieni Bwana kwa furaha.
Njoni mbele zake kwa kuimba; (K)

K) Mfanyieni Bwana shangwe, dunia yote.

2. Jueni kwamba Bwana ndiye Mungu;
Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake;
Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake. (K)

3. Kwa kuwa Bwana ndiye mwema;
Rehema zake ni za milele;
Na uaminifu wake vizazi na vizazi. (K)”

Injili. Yn 15:18-21

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu. Lakini haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye aliyenipeleka.

TAFAKARI

ULIMCHUKIA KRISTO, UTATUCHUKIA NA SISI PIA: Tupo ulimwenguni lakini hatupaswi kuwa wa ulimwengu. Kwa ubatizo wetu tumechaguliwa na Yesu tusiwe tena wa ulimwengu. Matendo yetu, maneno yetu, na namna yetu ya kuishi, havipaswi kufuata mawimbi ya ulimwengu huu. Tunapaswa kuwa mwanga pale ulimwengu unapokuwa giza, tunapaswa kuleta ladha ulimwenguni pale ulimwengu unapopoteza ladha. Haya yote ni kwenda kinyume na mkondo wa walimwengu wa sasa, na hivyo tukiendelea hivyo tuwe tayari kuchukiwa kwa matendo yetu yasiyoendana na ya walimwengu kwani matendo yetu yanapaswa kuwashitaki walimwengu. Tusife moyo kwani tunachota nguvu kutoka kwa Yesu kwani kama ulimwengu ulivyomchukia Kristo, utatuchukia sisi wafuasi wake pia. Watakatifu wengi walikubali kwenda kinyume na ulimwengu na malimwengu hata wakamwaga damu yao kwa ajili ya Kristo. Mtakatifu Karoli Lwanga na wenzake ni kielelezo hapa kwetu Afrika Mashariki jinsi walivyokubali kufa wakiishuhudia imani.

SALA: Ee Yesu nijalie uvumilivu katika magumu yaletwayo na Maisha ya ufuasi.

Masomo ya Misa Mei 3

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 03/05/2024

2024 MEI 3 : IJUMAA-JUMA LA TANO LA PASAKA

WAT. FILIPO NA YAKOBO, MITUME
Rangi: Nyekundu
Zaburi: Juma 1

Somo 1. 1 Kor 15:1-8

Ndugu zangu, nawaarifu ile Injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri; isipokuwa mliamini bure. Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alimtokea Kefa; tena na wale Thenashara; baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja; katika hao wengi wanaishi hata sasa, ila baadhi yao wamelala; baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote; na mwisho wa watu wote, alinitokea mimi, kama ni mtu aliyezaliwa si kwa wakati wake.

Wimbo wa Katikati. Zab 19:2-5

“1. Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu,
Na anga laitangaza kazi ya mikono yake.
Mchana husemezana na mchana,
Usiku hutolea usiku maarifa. (K)

K) Sauti yao imeenea duniani mwote.

2. Hakuna lugha wala maneno,
Sauti yao haisikilikani.
Sauti yao imeenea duniani mwote,
Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.
Katika hizo ameliwekea jua hema. (K)”

Injili. Yn 14:6-14

Yesu alimwambia Tomaso: Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba, tangu sasa mnamjua, tena mmemwona. Filipo akamwambia, Bwana, utuoneshe Baba, yatutosha. Yesu akamwambia, Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe wasemaje, Utuoneshe Baba? Husadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu? Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake. Mnisadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu; la! hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe. Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba. Nanyi mkiomba lolote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya Mwana. Mkiniomba neno lo lote kwa jina langu, nitalifanya.

SALA: Ee Yesu naomba unifungue macho yangu ya imani nimwone Baba kupitia wewe.

TAFAKARI

YESU NI NJIA YETU: Leo tunaadhimisha sikukuu ya watakatifu Filipo na Yakobo mitume. Hawa walitambua umuhimu wa maisha ya sadaka ili waweze kufika kwa Baba. Katika Injili tunaona kuwa Yesu ni Sakramenti ya Baba, yaani tunamwona Baba kupitia Yesu. Yesu anaposema yeye ni njia ya kwenda kwa Baba, hamaanishi kuwa yeye ni barabara tu bali anayetaka kwenda kwa Baba ni lazima aishi na kutenda kama Yesu. Yeye ni njia kwa kuwa yeye ndiye mlango wa kuingia na kutoka (Yn 10:9). Yeye ndiye ukweli kwani kwa kumtazama yeye tunamwona Baba. Yeye ni uzima kwani kwa kuishi kama yeye tunaungana na Baba anayetupa uzima. Swali la Philipo la kutamani kumwona Baba liwe tamanio letu sote ila tusimtafute Baba nje ya Yesu. Tumwone Baba katika Neno lake, katika Sakramenti zake, katika mamlaka funzi ya kanisa na katika nafsi ya kuhani mwadhimishaji wa mafumbo matakatifu ya imani yetu. Pia tumwone Baba katika mapokeo matakatifu yanayofunuliwa kwetu na Yesu Kristo.

Masomo ya Misa Mei 2

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 01/05/2024

2024 MEI 1 : JUMATANO-JUMA LA TANO LA PASAKA

Mt. Atanasi, Askofu na Mwalimu wa Kanisa
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 1

MTAKATIFU ATANASI WA ALEKSANDRIA

by Claretian Publications

Somo 1. Mdo 15:7-21

Wakati wa mtaguso wa Yerusalemu, baada ya hoja nyingi Petro alisimama, akawaambia, Ndugu zangu, ninyi mnajua ya kuwa tangu siku za kwanza Mungu alichagua miongoni mwenu ya kwamba Mataifa walisikie neno la Injili kwa kinywa changu na kuliamini. Na Mungu, ajuaye mioyo ya watu, akawashuhudia, akiwapa Roho Mtakatifu vile vile kama alivyotupa sisi; wala hakufanya tofauti kati yetu sisi na wao, akiwasafisha mioyo yao kwa imani. Basi sasa mbona mnamjaribu Mungu na kuweka kongwa juu ya shingo za wanafunzi, ambalo baba zetu wala sisi hatukuweza kulichukua. Bali twaamini kwamba tutaokoka kwa neema ya Bwana Yesu vile vile kama wao. Basi mkutano wote wakanyamaza, wakawasikiliza Barnaba na Paulo wakiwapasha habari za ishara na maajabu, ambayo Mungu aliyafanya kwa ujumbe wao katika Mataifa. Na hao walipokwisha kunyamaza Yakobo akajibu, akisema, Ndugu zangu, nisikilizeni. Simeoni ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya manabii yapatana na hayo, kama ilivyoandikwa. Baada ya mambo haya nitarejea, nami nitaijenga tena nyumba ya Daudi iliyoanguka. Nitajenga tena maanguko yake, nami nitaisimamisha; ili wanadamu waliosalia wamtafute Bwana, na mataifa yote ambao jina langu limetajwa kwao; asema Bwana, ajulishaye hayo tangu milele. Kwa sababu hiyo mimi naamua hivi; tusiwataabishe wale waliomgeukia Mungu katika mataifa; bali tuwaandikie kwamba wajiepushe na unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa, na damu. Kwa maana tangu zamani za kale Musa anao watu wahubirio mambo yake; katika kila mji husomwa kila Sabato katika masinagogi.

(K) Wahubirini mataifa habari za utukufu wake.

Wimbo wa Katikati. Zab 96:1-3, 10

“1. Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Mwimbieni Bwana nchi yote.
Mwimbieni Bwana, libarikini jina lake. (K)

2. Tangazeni wokovu wake siku kwa siku.
Wahubirini mataifa habari za utukufu wake,
Na watu wote habari za maajabu yake. (K)

3. Semeni katika mataifa, Bwana ametamalaki;
Naam, ulimwengu umethibitika usitikisike,
Atawahukumu watu kwa adili. (K) “

Injili. Yn 15:9-11

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Kama vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe.

TAFAKARI

UPENDO NI UKAMILIFU WA FURAHA YOTE: Upendo ni fadhila ya Kimungu inayotuwezesha kumpenda Mungu kuliko vitu vingine vyote na kumpenda jirani kama Kristo alivyotupenda. Katika Injili ya leo Yesu anatufundisha kuwa furaha ya kweli ipo katika kushika amri zake hususani amri ya upendo. Utambulisho wa Mkristo unapaswa kuoneshwa kwa njia ya upendo wa kweli. Kipimo cha upendo wa kweli ni Yesu mwenyewe na siyo mwanadamu. Agano la Kale linatufundisha kumpenda jirani kama nafsi (rej. Wal 19:1). Yesu anakamilisha amri hii kwa kutuonesha kuwa kipimo cha upendo wa kweli ni yeye. Kama alivyompenda Baba, nasi hatuna budi kupendana, vivyo hivyo. Upendo wa kweli unaweza kutenda mambo makubwa. Tushirikishane upendo wa Kristo kwa kuwajali wahitaji na kuwapatia mahitaji yao. Wajane Yatima, Wagane, Wagonjwa, Wafungwa ni makundi yanayotegemea kupata upendo wa pekee kutoka kwetu.

SALA: Ee Yesu naomba uniwashie fadhila ya mapendo.