Select Page

Masomo ya Misa Aprili 24

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 24/04/2024

2024 APRILI 24 : JUMATATU-JUMA LA NNE LA PASAKA

Mt. Fideli wa Stigmaringen, Padre na Shahidi
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 12:24, 13:5

Siku zile, neno la Bwana likazidi na kuenea. Na Barnaba na Sauli, walipokwisha kutimiza huduma yao, wakarejea kutoka Yerusalemu, wakamchukua pamoja nao Yohane aitwaye Marko. Na huko Antiokia katika Kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao. Basi watu hao, wakiisha kupelekwa na Roho Mtakatifu wakatelemkia Seleukia, na kutoka huko wakasafiri baharini hata Kipro. Na walipokuwa katika Salami wakalihubiri neno la Mungu katika masinagogi ya Mayahudi.

Wimbo wa Katikati. Zab 67:2-3, 5-6, 8

“1. Mungu na atufadhili na kutubariki,
Na kutuangazia uso wake.
Njia yake ijulike duniani,
Wokovu wake katikati ya mataifa yote. (K)

2. Mataifa na washangilie,
Naam, waimbe kwa furaha,
Maana kwa haki utawahukumu watu,
Na kuwaongoza mataifa walioko duniani. (K)

3. Watu na wakushukuru, Ee Mungu,
Watu wote na wakushukuru.
Mungu atatubariki sisi;
Miisho yote ya dunia itamcha Yeye. (K) “

(K) Watu na wakushukuru, Ee Mungu, Watu wote na wakushukuru.  

Injili. Yn 12:44-50

Siku ile Yesu alipaza sauti, Yeye aniaminiye mimi, haniamini mimi bali yeye aliyenipeleka. Naye anitazamaye mimi amtazama yeye aliyenipeleka. Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani. Na mtu akiyasikia maneno yangu, asiyashike, mimi simhukumu; maana sikuja ili niuhukumu ulimwengu, ila niuokoe ulimwengu. Yeye anikataaye mimi, asiyeyakubali maneno yangu, anaye amhukumuye; neno hilo nililolinena ndilo litakalomhukumu siku ya mwisho. Kwa sababu mimi sikunena kwa nafsi yangu tu; bali Baba aliyenipeleka, yeye mwenyewe ameniagiza nitakayonena na nitakayosema. Nami najua ya kuwa agizo lake ni uzima wa milele; basi hayo ninenayo mimi, kama Baba alivyoniambia, ndivyo ninenavyo.

SALA: Tunakuomba ewe Roho Mtakatifu utuwezeshe kuwa wasikivu kwa Kristo.

TAFAKARI

KAZI YA MUNGU LAZIMA ITENDEKE: Yesu anatualika tumsikie yeye na tutekeleze yale anayotuambia vinginevyo hali yetu mbeleni hatutabaki salama. Anataka kila mmoja wetu kazi ambayo kwayo Mungu alimuumba aitekeleze. Anatueleza kuwa maneno aliyotuambia ni kutoka kwa Baba yake na sio yake. Maneno haya ndiyo yaliyowapa nguvu mitume kokote walikotawanyikia, (rej. somo 1), “siku zile Neno la Bwana likazidi na kuenea…na Barnaba na Sauli wakatengwa kwa kazi ile waliyoitiwa.” Hapa tunaona jinsi mitume walivyohangaika kuhakikisha kuwa utume wa Kanisa unaendelea. Mtume Paulo anaeleza tabia za mtu anayeendeleza kazi hii ya kusambaza Neno la Mungu kwamba “awe mtu asiyeshtakiwa kwa neno, asijipendekeze, asitafute maslahi binafsi, asipende mapato ya aibu, awe mkaribishaji, mpenda mema, mwenye kiasi…” (Tit 1:7-9). Hivi ni vielelezo vya kumsaidia mtu katika utume na anajikuta anautekeleza vyema, na hii itamsaidia kuwa msikivu kwa sauti ya Kristo anayetuhabarisha habari toka kwa Baba yake wa mbinguni.

 

Masomo ya Misa Aprili 23

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 23/04/2024

2024 APRILI 23 : JUMATATU-JUMA LA NNE LA PASAKA

Mt. Georgi, Shahidi
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 11:19-26

Siku zile, wale waliotawanyika kwa sababu ya ile dhiki iliyotukia kwa habari ya Stefano, wakasafiri hata Foinike na Kipro na Antiokia, wasilihubiri lile neno ila kwa Wayahudi peke yao. Lakini baadhi ya hao walikuwa watu wa Kipro na Kirene, nao walipofika Antiokia wakasema na Wayahudi wa Kiyunani, wakihubiri Habari Njema za Bwana Yesu. Mkono wa Bwana ukawa pamoja nao; watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana. Habari hizo za watu hao zikafika masikioni mwa Kanisa lililokuwako katika Yerusalemu; wakamtuma Barnaba, aende hata Antiokia. Naye, alipokwisha kufika na kuiona neema ya Mungu akafurahi, akawasihi wote waambatane na Bwana kwa kusudi la moyo. Maana alikuwa mtu mwema amejaa Roho Mtakatifu na imani; watu wengi wakaongezeka upande wa Bwana. Kisha akatoka akaenda Tarso kumtafuta Sauli; hata alipokwisha kumwona akamleta Antiokia. Ikawa kwa muda wa mwaka mzima wakakusanyika pamoja na Kanisa na kuwafundisha watu wengi. Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza hapo Antiokia.

(K) Enyi mataifa yote, msifuni Bwana.

Wimbo wa Katikati. Zab 87:1-7

“1. Msingi wake upo
Juu ya milima mitakatifu.
Bwana ayapenda malango ya Sayuni
Kuliko maskani zote za Yakobo.
Umetajwa kwa mambo matukufu,
Ee Mji wa Mungu. (K)

2. Nitataja Rahabu na Babeli
Miongoni mwao wanaonijua.
Tazama Filisti, na Tiro, na Kushi;
Huyu alizaliwa humo.
Naam, mintarafu Sayuni itasemwa,
Huyu na huyu walizaliwa humo. (K)

3. Na Yeye Aliye juu
Ataufanya imara.
Bwana atahesabu, awaandikiapo mataifa,
Huyu alizaliwa humo.
Waimbao na wachezao na waseme,
Visima vyangu vyote vimo mwako. (K)”

Injili. Yn 10: 22-30

Huko Yerusalemu ilikuwa Sikukuu ya Kutabaruku; ni wakati wa baridi. Naye Yesu alikuwa akitembea hekaluni, katika ukumbi wa Sulemani. Basi Wayahudi walimzunguka, wakamwambia, Hata lini utatuhangaisha nafsi zetu? Kama wewe ndiwe Kristo, utuambie waziwazi. Yesu akawajibu, Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia. Lakini ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu. Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu. Mimi na Baba tu umoja.

TAFAKARI

Huko Yerusalemu ilikuwa Sikukuu ya Kutabaruku; ni wakati wa baridi. Naye Yesu alikuwa akitembea hekaluni, katika ukumbi wa Sulemani. Basi Wayahudi walimzunguka, wakamwambia, Hata lini utatuhangaisha nafsi zetu? Kama wewe ndiwe Kristo, utuambie waziwazi. Yesu akawajibu, Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki. Kazi hizi ninazozifanya kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia. Lakini ninyi hamsadiki, kwa sababu hammo miongoni mwa kondoo wangu. Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu. Mimi na Baba tu umoja.

 

Masomo ya Misa Aprili 22

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 22/04/2024

2024 APRILI 22 : JUMATATU-JUMA LA NNE LA PASAKA

Mt. Konrad wa Parzam, Mtawa Mfransisko
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 11:1-18

Siku zile, mitume na ndugu waliokuwako katika Uyahudi wakapata habari ya kwamba watu wa Mataifa nao wamelipokea neno la Mungu. Na Petro alipopanda kwenda Yerusalemu, wale walio wa tohara wakashindana naye, wakisema, Uliingia kwa watu wasiotahiriwa ukala nao. Petro akaanza kuwaeleza kwa taratibu, akasema, Nalikuwa katika mji wa Yafa, nikiomba, roho yangu ikazimia, nikaona maono; chombo kinashuka, kama nguo kubwa inatelemshwa kutoka mbinguni kwa pembe zake nne, kikanifikia. Nikakitazama sana, nikifikiri, nikaona wanyama wa nchi wenye miguu minne, na wanyama wa mwituni, nao watambaao, na ndege wa angani. Nikasikia na sauti ikiniambia, Ondoka; Petro, ukachinje ule. Nikasema, Hasha, Bwana, kwa maana kitu kilicho kichafu au kilicho najisi hakijaingia kabisa kinywani mwangu. Sauti ikanijibu mara ya pili kutoka mbinguni, alivyovitakasa Mungu, usivinene wewe najisi. Jambo hili likatendeka mara tatu, kisha vitu vyote vikavutwa tena juu mbinguni. Na tazama, mara hiyo watu watatu wakasimama mbele ya nyumba tuliyokuwamo waliotumwa kwangu kutoka Kaisaria. Roho akaniambia nifuatane nao, nisione tashwishi. Ndugu hawa sita nao wakaenda nami, tukaingia katika nyumba ya mtu yule; akatueleza jinsi alivyomwona malaika aliyesimama nyumbani mwake na kumwambia, tuma watu kwenda Yafa ukamwite Simoni aitwaye Petro, atakayekuambia maneno ambayo yatakuokoa, wewe na nyumba yako yote. Ikawa nilipoanza kunena, Roho Mtakatifu akawashukia kama alivyotushukia sisi mwanzo. Nikalikumbuka neno lile la Bwana, jinsi alivyosema, Yohane alibatiza kwa maji kweli, bali ninyi mtabatiza kwa Roho Mtakatifu. Basi, ikiwa Mwenyezi Mungu amewapa wao karama ile ile aliyotupa sisi tuliomwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani niweze kumpinga Mungu? Waliposikia maneno haya wakanyamaza, wakamtukuza Mungu, wakisema, Basi, Mungu amewajalia hata mataifa nao toba liletalo uzima.

Wimbo wa Katikati. Zab 42:2-3.43:3-4

“1. Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji,
Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, ee Mungu. (K)

2. Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai,
Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu? (K)

3. Nilitewe nuru yako na kweli yako ziniongoze,
zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu na hata maskani yako. (K)

4. Hivyo nitakwenda madhabahuni kwa Mungu,
kwa Mungu aliye furaha yangu na shangwe yangu;
Nitakusifu kwa kinubi, ee Mungu, Mungu wangu. (K)”

K) Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai.  
K) Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai.  

Injili. Yn 10: 1-10

Yesu alisema: Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo. Mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwamwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia; na mbwamwitu huwakamata na kuwatawanya. Yule hukimbia kwa kuwa ni mtu wa mshahara; wala mambo ya kondoo si kitu kwake. Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo. Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja. Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.

TAFAKARI

YESU NI MCHUNGAJI WETU: Kanisa Katoliki limekabidhiwa jukumu la kuwaelekeza watu wote kumjua Mungu. Katekisimu ya Kanisa Katoliki inasema, “Sakramenti ya ubatizo ndiyo inayomwondolea mtu dhambi ya Asili pamoja na dhambi nyinginezo, kutupatia neema ya utakaso, kutuandika watoto wa Mungu na wa Kanisa.” Ni kwa sakramenti hii tunaanza safari ya kuwa kondoo na tunapaswa kuwa chini ya mchungaji wetu Yesu Kristo. Kanisa linapaswa kuelewa kuwa, lina wajibu si tu wa kuwalinda walio ndani bali hata kuwatafuta na kuwarudisha waliopotea, (walegevu). Ukiangalia mfumo tulionao sasa wa Jumuiya Ndogondogo za Kikirsto utagundua kwa urahisi sana ni wapi kuna shida katika kuiishi imani yetu. Haitoshi kusubiri mpaka mtu afe na fomu yake kujazwa kuwa ‘hastahili kufanyiwa maziko ya Kikristo’’ kutokana na namna yake alivyokuwa anaishi. Injili hii inatutaka tumrekebishe kabla na hii ni kazi yetu sote, sio suala la kusema ni kazi ya mapadre/maaskofu la hasha, kila mbatizwa anapaswa kumlinda mwenzake, kuwa mchunguji mwema kama Kristo mwenyewe.

SALA: Ee Mungu utujalie tutambue wajibu wa kuwaongoza walio walegevu kiimani.

Masomo ya Misa Aprili 21

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 21/04/2024

2024 APRILI 21 : DOMINIKA YA NNE YA PASAKA

Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 4

Somo 1. Mdo 4:8-12

Ndipo Petro, akijaa Roho Mtakatifu, aliwaambia, Enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli, kama tukiulizwa leo habari ya jambo jema alilofanyiwa yule mtu dhaifu, jinsi alivyoponywa, jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.

(K) Jiwe walilokataa waashi, Limekuwa jiwe kuu pembeni. 

Wimbo wa Katikati. Zab 118: 1,8-9, 21-23, 26, 28,29

“1. Aleluya.
Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni Mwema,
Kwa maana fadhili zake ni za milele.
Ni heri kumkimbilia Bwana
Kuliko kuwatumainia wanadamu
Ni heri kumkimbilia Bwana
Kuliko kuwatumainia wakuu. (K)

2. Nitakushukuru kwa maana umenijibu,
Nawe umekuwa wokovu wangu.
Jiwe walilolikataa waashi
Limekuwa jiwe kuu la pembeni.
Neno hili limetoka kwa Bwana,
Nalo ni ajabu machoni petu. (K)

3. Na abarikiwe yeye ajaye kwa jina la Bwana;
Tumewabarikia toka nyumbani mwa Bwana.
Ndiwe Mungu wangu, nami nitakushukuru,
Ndiwe Mungu wangu, nami nitakutukuza.
Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema,
Kwa maana fadhili zake ni za milele. (K)”

Somo 2. 1 Yoh 3:1-2

Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye. Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo.

Injili. Yn 10: 11-18

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mimi ndimi mchungaji mwema, Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo. Mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwamwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia; na mbwamwitu huwakamata na kuwatawanya. Yule hukimbia kwa kuwa ni mtu wa mshahara; wala mambo ya kondoo si kitu kwake. Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya Kondoo. Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja. Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.

TAFAKARI

“KRISTO MCHUNGAJI MWEMA: KIELELEZO CHA KUITIKIA WITO
Leo ni Dominika ya Kristo Mchungaji Mwema ambapo mama Kanisa anatualika kuiombea miito mitakatifu. Wito wowote ni matokeo ya ndoto anayokuwa nayo mtu katika maisha yake; jambo gani ambalo ana hamu nalo. Katika maisha ya Mtakatifu Yosefu tunaona jinsi ambavyo ndoto zetu zinaundwa katika Mungu na hivyo kumwezesha mmoja kutimiza kile ambacho ni kweli mpango wa Mungu kwake. Hili linahitaji utayari na kuweka maisha ya mmoja rehani. Kuwa tayari kuacha kujisikiliza na kumapatia Mungu nafasi aseme na wewe.
Katika somo la kwanza Mchungaji Mwema aliye msingi na chemchemi ya miito yote amejionesha kama jiwe kuu la pembeni. Hii inamaanisha kwamba ni yeye anayeshikilia uimara wa kundi lake; kwa mafundisho yake, kwa uponyaji wake na kwa kuwamiminia neema kutoka mbinguni. Hivyo daima yupo na kundi lake na kukosekana kwake ni sawa na maangamizi kwa kundi. Ingawa alidharaulika na watu wa ulimwengu, wakiwakilishwa na Wayahudi lakini yeye ambaye ni “Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni.” Mchungaji ambaye ni wa kuajiriwa “kondoo si mali yake…huwaacha kondoo na kukimbia; na mbwa-mwitu huwakamata na kuwatawanya.” Mchungaji mwema kondoo ni mali yake. Daima anakaa nao kama jiwe kuu la pembeni na ni msingi wake imara.
Huduma na utumishi wetu kwa wenzetu inapata ufanisi pale tunapoona kuwa tukifanyacho ni sehemu muhimu si kwa uwepo wangu au si sehemu muhimu kwa uhai wangu tu bali hata kwa wale ninaowahudumia; pale tutakapoweza kubadili mawazo ya kutumia nafasi mbalimbali tulizonazo kwa ajili ya kujinufaisha binafsi na hivyo kutafuta kujinufaisha wote. Ni hali ya kuwa tayari kujifunua na kuwaangalia wengine walio pembeni yangu; hali ya kuona kuwajibika kwa mwenzangu kwa sababu yu sehemu muhimu na anayeleta maana ya uwepo wangu. Ni hatua muhimu kuelekea undugu wa kikristo ambao Kristo anakuwa kwetu ndugu yetu wa kwanza na katika yeye sote tunafanywa kuwa ndugu.
Mtume Yohane katika somo la pili anatupeleka hatua moja mbele. Kristo Mchungaji Mwema aliutwaa ubinadamu wetu na hivyo kwa fumbo la Umwilisho nasi tunafanyika kuwa wana wa Mungu. Ni tendo la upendo mkubwa wa Mungu kwetu. Hivyo nasi tunafanywa kwa namna fulani kuwa kama Yeye Mchungaji Mwema au Jiwe Kuu la pembeni. Hapo ndipo tunapoona wito wetu ambao unajikita katika fumbo zima la Kristo Mfufuka. Kwa namna nyingine hapa tunaona muunganiko wa Dominika hii na jukumu la kuiombea miito. Zawadi hii ya kufanyika kuwa wana wa Mungu kimantiki inaathiri pia utendaji wetu. Bila shaka utajimithilisha na Yeye, Kristo Mchungaji Mwema ambaye kwa njia yake tunafanyika kuwa wana wa Mungu. Hivyo, ni vema kujitafakari vyema katika sauti ya Mungu inayoita na kuitikia vema kusudi kuleta matunda yanayotarajiwa na Yeye anayetuita.
Kristo Mchungaji Mwema ni kielelezo, chanzo na uhai wa wito huo. Yeye aliye Njia, Ukweli na Uzima (rej. Yoh 14:6) anatuonesha jinsi nasi tunavyopaswa kuwa kama Yeye katika kutekeleza majukumu yetu mbalimbali tuliyoaminishwa kwayo kadiri ya wito wa Mungu. Kwanza kwa kuwa tayari kujitoa kwa ajili ya unaowahudumia. Ni wito kwa viongozi wa kada zote kuiga mfano wake; zaidi anaonesha kwa kuwajua watu wake, yaani, mahitaji yao, vipaji vyao, udhaifu wao na hivyo kila mmoja atawaongoza kwa namna yake mahsusi. Yeye pia ni chanzo kwani ni ufunuo wa Mungu kwetu; tunapoitikia wito wetu tunapaswa kuchota kutoka kwake yale tunayopaswa kuyatekeleza; tunapaswa kuisikiliza sauti yake. Lakini pia Yeye ni uhai wa kondoo wake. Anakuwa ni nguvu ya kuwaongoza wengine kufikia ukamilifu. Hivyo Yeye aliye Mchungaji mwema anatuita sisi kuitikia miito yetu mbalimbali, kila mmoja kwa kadiri yake na kumwakilisha Yeye kwa kujimithilisha katika haiba yake ya Mchungaji Mwema. Kwa njia hiyo tutashiriki nasi katika kuuokoa ubinadamu.”

SALA: Ee Yesu utujalie wachungaji wema watakaotuongoza kwenye malisho mema na hatimaye tufike kwako mbinguni.

Maomo ya Misa Aprili 20

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 20/04/2024

2024 APRILI 20 : JUMAMOSI-JUMA LA TATU LA PASAKA

Mt. Marselino wa Embrun, Askofu
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 3

Somo 1. Mdo 9:31-42

Kanisa lilipata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likiendelea na kuongezeka katika kicho cha Bwana, na faraja ya Roho Mtakatifu. Hata Petro alipokuwa akizunguka-zunguka pande zote akawatelemkia na watakatifu waliokaa Lida. Akamwona mtu mmoja huko, jina lake Ainea, mtu huyo amelala kitandani miaka minane; maana alikuwa amepooza. Petro akamwambia, Ainea, Yesu Kristo akuponya; ondoka, ujitandikie. Mara akaondoka. Na watu waliokaa Lida na Sharani wakamwona, wakamgeukia Bwana. Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa. Ikawa siku zile akaugua, akafa; hata walipokwisha kumwosha, wakamweka orofani. Na kwa kuwa mji wa Lida ulikuwa karibu na Yafa, nao wanafunzi wamesikia ya kwamba Petro yuko huko, wakatuma watu wawili kwake, kumsihi na kusema, Usikawie kuja kwetu. Petro akaondoka akafuatana nao. Alipofika, wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao. Petro akawatoa nje wote, akapiga magoti, akaomba, kisha akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. Akampa mkono, akamwinua, hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai. Ikajulikana katika mji mzima wa Yafa; watu wengi wakamwamini Bwana.

Wimbo wa Katikati. Zab 116:12-17

“1. Nimrudishie Bwana nini
Kwa ukarimu wake wote alionitendea?
Nitakipokea kikombe cha wokovu;
Na kulitangaza jina la Bwana. (K)

2. Nitaziondoa nadhiri zangu kwa Bwana,
Naam, mbele ya watu wake wote.
Ina thamani machoni pa Bwana
Mauti ya wacha Mungu wake. (K)

3. Ee Bwana, hakika mimi ni mtumishi wako,
Mtumishi wako, mwana na mjakazi wako,
Umenifungua vifungo vyangu.
Nitakutolea dhabihu ya kushukuru;
Na kulitangaza jina la Bwana. (K)”

K) Nimrudishie Bwana nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?

Injili. Yn 6:60-69​

Siku ile, watu wengi miongoni mwa wanafunzi wake waliposikia maneno ya Yesu juu ya mkate wa uzima, walisema: Neno hili ni gumu, ni nani awezaye kulisikia? Naye Yesu akafahamu nafsini mwake ya kuwa wanafunzi wake wanalinung’unikia neno hilo, akawaambia, Je, neno hili linawakwaza? Itakuwaje basi, mmwonapo Mwana wa Adamu akipaa huko alikokuwako kwanza? Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima. Lakini kuna wengine miongoni mwenu wasioamini. Kwa maana Yesu alijua tangu mwanzo ni nani wasioamini, naye ni nani atakayemsaliti. Akasema, Kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu. Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma, wasiandamane naye tena. Basi Yesu akawaambia wale Thenashara, Je! ninyi nanyi mwataka kuondoka? Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.

TAFAKARI

KWA YESU KUNA UZIMA: Kukiri kwa Petro kama tulivyosikia katika Injili “Bwana twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele” ni kielelezo tosha kuwa Kristo ni mweza wa yote, kutangatanga kwetu huku na kule kutafuta usalama hakutusaidii kitu. Hata hivyo ili kumfuata Yesu kikamilifu hatuna budi kuyaacha malimwengu (rej. Mt 19:16-22) na kuwajali wahitaji. Tukiishi hivi tunakamilika na kuishi maisha matakatifu. Ndilo hili Petro alifanya, kuwajali wahitaji: alimponya Aimea na alimfufua Dorkasi, kwa kuyafanya haya alifanya watu wengi wakamwongokea Mungu. Utume unaofanywa na Kanisa ni wa kujisadaka hasa kwa ajili ya wengine. Yesu aliwahoji wale Thenashara, “Je ninyi nanyi mwataka kuondoka?” Nasi leo tunaulizwa swali hili hili, ‘Je tunataka kuondoka? tunataka kuhama toka Katoliki na kwenda dini/madhehebu mengine?’ Perto anatusaidia kutambua kwamba kwa Yesu kuna mzima. Hivyo tumsadiki (Yesu) na kumfuata ili atufanye watakatifu.

SALA: Ee Yesu utusaidie tutambue kwamba kwako kuna uzima wetu.