Select Page

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 19/04/2024

2024 APRILI 19 : IJUMAA-JUMA LA TATU LA PASAKA

Mt. Leo wa IX, Papa
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Juma 3

Somo 1. Mdo 9:1-20

Siku zile, Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana, akamwendea kuhani mkuu, akataka ampe barua za kwenda Dameski zilizoandikwa kwa masinagogi, ili akiona watu wa njia hii, waume kwa wake, awafunge na kuwaleta Yerusalemu. Hata alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi? Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe. Lakini simama, uingie mjini, nawe utaambiwa yakupasayo kutenda. Na wale watu waliosafiri pamoja naye wakasimama kimya, wakiisikia sauti, wasione mtu. Sauli akainuka katika nchi, na macho yake yalipofumbuka, hakuona kitu; wakamshika mkono wakamleta mpaka Dameski. Akawa siku tatu haoni; hali, wala hanywi. Basi palikuwapo Dameski mwanafunzi jina lake Anania. Bwana akamwambia katika maono, Anania. Akasema, Mimi hapa, Bwana. Bwana akamwambia, Simama, enenda zako katika njia iitwayo Nyofu, ukaulize katika nyumba ya Yuda mtu aitwaye Sauli, wa Tarso; maana, angalia, anaomba; naye amemwona mtu, jina lake Anania, akiingia, na kumwekea mikono juu yake, apate kuona tena. Lakini Anania akajibu, Bwana, nimesikia habari za mtu huyu kwa watu wengi, mabaya mengi aliyowatenda watakatifu wako Yerusalemu; hata hapa ana amri itokayo kwa wakuu wa makuhani awafunge wote wakuitiao Jina lako. Lakini Bwana akamwambia, Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli. Maana nitamwonesha yalivyo mengi yatakayompasa kuteswa kwa ajili ya Jina langu. Anania akaenda zake, akaingia mle nyumbani, akamwekea mikono akisema, Ndugu Sauli, Bwana amenituma, Yesu, yeye aliyekutokea katika njia uliyoijia, upate kuona tena, Ukajazwe Roho Mtakatifu. Mara vikaanguka machoni pake vitu kama magamba, akapata kuona, akasimama, akabatizwa, akala chakula, na kupata nguvu. Akawa huko siku kadha wa kadha pamoja na wanafunzi walioko Dameski. Mara akamhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba yeye ni Mwana wa Mungu.

K) “Enendeni ulimwenguni mwote,
mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe.

Wimbo wa Katikati. Zab 117

“1. Enyi mataifa yote, msifuni Bwana,
Enyi watu wote, mhimidini. (K)

2. Maana fadhili zake kwetu sisi ni kuu,
Na uaminifu wa Bwana ni wa milele (K)”

Injili. Yn 6:52-59

Siku ile, Wayahudi walishindana wao kwa wao wakisema, Awezaje mtu huyu kutupa sisi mwili wake ili tuule? Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi. Hiki ndicho chakula kishukacho kutoka mbinguni; si kama mababa walivyokula, wakafa; bali akilaye chakula hicho ataishi milele. Maneno hayo aliyasema katika sinagogi, alipokuwa akifundisha, huko Kapernaumu.

TAFAKARI

WONGOFU NI HATUA: Mama Kanisa leo anatupatia nafasi ya kutafakari kuongoka kwake Sauli (Mdo 9:1-20). Sauli alikuwa mmoja kati ya watesaji wakuu wa Kanisa la mwanzo. Ni katika mojawapo za safari za kuwatesa Wakristo, Sauli anaangazwa na mwanga kutoka angani (kiasi cha kupelekea Sauli kuwa kipofu) na sauti ikimuuliza “Sauli! Sauli! Kwa nini unanitesa?”(Mdo 9:4). Simulizi inaeleza jinsi Anania alivyotumwa kwenda kumponya Sauli na hatimaye kuongoka kwake. Na baada ya hapo Sauli “Akaanza kuhubiri katika masunagogi kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu”(Mdo 9:20). Swali: Je! Kina Sauli wameisha? Jibu ni hapana. Kwani kuna watu na makundi mengi yanayolidhulumu Kanisa na waumini wake. Hata maisha yetu kinyume na mafundisho ya Kristo ni kulitesa Kanisa. Je! Unadhani maneno ya Yesu kwamba “Mimi ni Yesu ambaye wewe unamtesa” hayakuhusu? Tafakari na chukua hatua.

SALA: Ee Mungu utupe neema ya kusimama imara hata katika madhulumu.