Select Page

Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 03/04/2024

2024 APRILI 3 : JUMATANO-JUMA LA KWANZA LA PASAKA

Mt. Agape
Rangi: Nyeupe
Zaburi: Tazama sala ya siku

“Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilichonacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende.”

Somo 1. Mdo 3:1-10

Petro na Yohane walikuwa wakikwea pamoja kwenda hekaluni, saa ya kusali, saa tisa Na mtu mmoja aliyekuwa kiwete toka tumboni mwa mamaye alichukuliwa na watu, ambaye walimweka kila siku katika mlango wa hekalu uitwao mzuri, ili aombe sadaka kwa watu waingiao ndani ya hekalu. Mtu huyu akiwaona Petro na Yohane wakiingia hekaluni aliomba apewe sadaka. Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohane, akasema, Tutazame sisi. Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilichonacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende. Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu. Akaondoka upesi akasimama, akaanza kwenda; akaingia ndani ya hekalu pamoja nao, akienda, akiruka-ruka, na kumsifu Mungu. Watu wote wakamwona akienda, akimsifu Mungu. Wakatambua, ya kuwa yeye ndiye aliyekuwa akiketi na kuomba sadaka penye mlango Mzuri wa hekalu; wakajaa ushangao wakastaajabia mambo yale yaliyompata.

Wimbo wa Katikati. Zab 105:1-4, 6-9

“1. Mshukuruni Bwana, liitieni jina lake,
Wajulisheni watu matendo yake,
Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi,
Zitafakarini ajabu zake zote. (K)

K) Bwana anajaza nchi na fadhili zake.

2. Jisifuni kwa jina lake takatifu,
Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana.
Mtakeni Bwana na nguvu zake,
Utafuteni uso wake sikuzote. (K)

3. Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake;
Enyi wana wa Yakobo, wateule wake.
Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu;
Duniani mwote mna hukumu zake. (K)

4. Analikumbuka agano lake milele;
Neno lile aliloviamuru vizazi elfu.
Agano alilofanya na Ibrahimu,
Na uapo wake kwa Isaka. (K) “

Injili. Lk 24:14-35

Siku ile ile watu wawili miongoni mwao walikuwa wakienda kijiji kimoja, jina lake Emau, kilichokuwa mbali na Yerusalemu kama mwendo wa saa mbili. Nao walikuwa wakizungumza wao kwa wao habari za mambo hayo yote yaliyotukia. Ikawa katika kuzungumza na kuulizana kwao, Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao. Macho yao yakafumbwa wasimtambue. Akawaambia, Ni maneno gani haya mnayosemezana hivi mnapotembea? Wakasimama wamekunja nyuso zao. Akajibu mmoja wao, jina lake Kleopa, akamwambia, Je! Wewe peke yako u mgeni katika Yerusalemu, hata huyajui yaliyotukia humo siku hizi? Akawauliza, Mambo gani? Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote;

tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli. Zaidi ya hayo yote, leo ni siku ya tatu tangu yalipotendeka mambo hayo; tena, wanawake kadha wa kadha wa kwetu walitushitusha, waliokwenda kaburini asubuhi na mapema, wasiuone mwili wake; wakaja wakasema ya kwamba wametokewa na malaika waliosema kwamba yu hai. Na wengine waliokuwa pamoja nasi walikwenda kaburini wakaona vivyo hivyo kama wale wanawake walivyosema, ila yeye hawakumwona. Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je, haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake? Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe. Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, naye alifanya kama anataka kuendelea mbele. Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao. Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao. Wakaambiana, Je! Mioyo yetu haikuwaka ndani yetu hapo alipokuwa akisema nasi njiani, na kutufunulia maandiko? Wakaondoka saa ile ile, wakarejea Yerusalemu, wakawakuta wale kumi na mmoja wamekutanika, wao na wale waliokuwa pamoja nao, wakisema, Bwana amefufuka kweli kweli, naye amemtokea Simoni. Nao waliwapa habari ya mambo yale ya njiani, na jinsi alivyotambulikana nao katika kuumega mkate.

TAFAKARI

DAIMA UKARIMU UNA FAIDA: Kuna mwanasaikolojia anaitwa Delno Tromp alisema, “urafiki wa kweli ni kushirikishana hata tone la mwisho la maji wakati huna uhakika wa maji mengine.” Hawa wanafunzi wa Emau walimkirimu Yesu kwa kumkaribisha ili ale nao chakula cha jioni bila hata kujua ni Yesu. Walifanya vile kama binadamu tu, lakini matokeo yake Yesu akajifunua kwao na kuwaonesha kuwa ukarimu wao umewaneemesha. Hata Petro na Yohane nao katika somo la kwanza, walimkirimu yule kiwete kwa kumponya na wakamfanya afurahie maisha yake. Jamii yetu leo inakosa ukarimu, wenye nacho wanakosa majitoleo na huruma kwa wasio nacho. Sehemu nyingine imani potofu zimepelekea watu kutosaidiana katika shida kwani ukimsaidia mtu halafu mbeleni akapata taabu, uliyesaidia unaanza kutiliwa shaka, mara anataka amtoe kafara (sadaka-msukule) n.k. Tunasahau kuwa Mungu anatutaka tusaidiane.

SALA: Ee Kristo Mfufuka, utujalie moyo wa ukarimu wa kipasaka.