Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 12/10/2024

2024 OKTOBA 12: JUMAMOSI-JUMA LA 27 LA MWAKA

Mt. Wilfridi wa York, Askofu
Rangi: Kijani

Zaburi: Juma III

SOMO 1. Gal 3:22-29

Andiko limeyafunga yote chini ya nguvu ya dhambi, makusudi hao waaminio wapewe ile ahadi kwa imani ya Yesu Kristo. Lakini kabla ya kuja ile imani tulikuwa tumewekwa chini ya sheria, tumefungwa mpaka ije ile imani itakayofunuliwa. Hivyo torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani. Lakini, iwapo imani imekuja, hatupo tena chini ya kiongozi. Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa Mungu kwa njia ya imani katika Kristo Yesu. Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu. Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.

WIMBO WA KATIKATI. Zab 105: 2-7

1. Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi,
Zitafakarini ajabu zake zote.
Jisifuni kwa jina lake takatifu,
Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana.

(K) Bwana analikumbuka agano lake milele.

2. Mtakeni Bwana na nguvu zake,
Utafuteni uso wake sikuzote.
Zikumbukeni ajabu zake alizozifanya,
Miujiza yake na hukumu za kinywa chake. (K)

3. Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake,
Enyi wana wa Yakobo, wateule wake.
Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu;
Duniani mwote mna hukumu zake. (K)

INJILI. Lk 11:27-28

Ikawa, Yesu alipokuwa akisema, mwanamke mmoja katika mkutano alipaza sauti yake, akamwambia, “Heri tumbo lililokuzaa, na matiti uliyonyonya.” Lakini yeye alisema, “Afadhali, heri walisikiao neno la Mungu na kulishika.”

TAFAKARI

KUIVUNJA SHERIA: Sababu moja inayofanya tushindwe katika jaribio la kuhubiri Habari Njema kwa wengine ni kule kusita au kuogopa kupandikiza na kuifanya sheria ikue katika maisha ya wale tunaowahubiria. Tunachofikiri ni kwamba dhamiri zao zinatosha kuwafanya wakiri dhambi zao na kumuhitaji Mungu kama suluhisho lao. Kifupi tunaacha waongozwe na dhamira zao. Kwa hiyo tunaishia kujenga malumbano au hoja na watu ambao matumaini yao ni kwamba wao sio waovu kama walivyo watu wengine. Tunajenga hoja na watu wanaosema kwamba uelewa wao juu ya Mungu unawafanya wafaulu katika maadili. Lakini ikiwa tutawaongoza katika Amri Kumi za Mungu, moja baada ya nyingine, na kuwaambia wayapime maisha yao kulingana na viwango alivyoweka Mungu, tutawafanya waone mwanga mpya katika Injili. Mara nyingi hatutaki uhuru unaopatikana katika Kristo, hadi pale tunapopata uelewa wa kina kuhusu utumwa wetu wa dhambi na hukumu ya Mungu.

SALA: Bwana Yesu utujalie tutambue kwamba sheria yako ni kamilifu.