Tumsifu Yesu Kristo. Karibu Katika Masomo ya Misa 18/10/2024

2024 OKTOBA 18: IJUMAA: JUMA LA 28 LA MWAKA

MT. LUKA, MWINJILI
Rangi: Nyekundu

Zaburi: Tazama Sala ya Siku

SOMO 1. 2 Tim 4:10-17

Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia. Luka peke yake yupo hapa pamoja nami. Umtwae Marko, umlete pamoja nawe maana anifaa kwa utumishi. Lakini Tikiko nalimpeleka Efeso. Lile joho nililoliacha kwa Karpo huko Troa, ujapo ulilete, na vile vitabu hasa vile vya ngozi. Iskanda,  mfua shaba, alionyesha ubaya mwingi kwangu; Bwana atamlipa sawasawa na matendo yake. Nawe ujihadhari na huyo, kwa sababu aliyapinga sana maneno yetu. Katika jawabu langu la kwanza hakuna mtu aliyesimama upande wangu, bali wote waliniacha; naomba wasihesabiwe hatia kwa jambo hilo. Lakini Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu, ili kwa kazi yangu ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu, hata wasikie mataifa yote.

WIMBO WA KATIKATI. Zab 145:10-13, 17-18

1. Ee Bwana, kazi zako zote zitakushukuru,
Na wacha Mungu wako watakuhimidi.
Wataunena utukufu wa ufalme wako,
Na kuuhadithia uweza wako.

(K) “Wacha wako, Ee Bwana, wajulisha matendo yako makuu na utukufu wa fahari ya ufalme wako.

2. Ili kuwajulisha watu matendo yake makuu,
Na utukufu wa fahari ya ufalme wake.
Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote,
Na mamlaka yako ni ya vizazi vyote. (K)

3. Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote,
Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
Bwana yu karibu na wote wamwitao,
Wote wamwitao kwa uaminifu. (K)

INJILI. Lk 10:1-9

Bwana aliweka wengine, sabini, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe. Akawaambia, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Enendeni; angalieni, nawatuma kama wana-kondoo kati ya mbwa-mwitu. Msichukue mfuko, wala mkoba, wala viatu; wala msimwamkie mtu njiani. Na nyumba yo yote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu; na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la, hayumo, amani yenu itarudi kwenu. Basi, kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake. Msihame-hame kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii. Na mji wo wote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu; wapozeni wagonjwa waliomo, waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia.

TAFAKARI

MBWA MWITU, UMISIONARI NA PESA: Yesu anatutahadharisha kuhusu mapingo. Mbwa mwitu wanaotupinga wanakuja katika namna nyingi. Wako wanaotupinga kiroho, hawa wanalishambilia kwa ukali kabisa Kanisa, hasa katika uvumilivu, upole, na usafi wa moyo. Baadhi ya wale wanaotupinga wanaonekana kuwa watakatifu hata kuliko jinsi sisi tulivyo, lakini mtawatambua kwa matunda yao. Kumtumikia Mungu katika zama hizi kunahitaji ujasiri na uvumilivu katika maumivu, na utambuzi katika wale wanaotushambulia. Tunapaswa kusali kusudi tuweze kukua katika fadhila, na kutafuta namna ya kutambua na kuelewa mapingamizi tunayokutana nayo. Je! Wachungaji wafikirie kuhusu mshahara watakaolipwa wanapotaka kufanya kazi? Wafuasi wanapaswa kumtumainia Mungu kwa mahitaji yao, na kujitoa zaidi kwa utume wao. Wanaweza wakaonekana kuwa matajiri kwa sababu wana viatu miguuni lakini jambo la msingi ni kwamba mali haipaswi kuwa ndio kipaumbele. Mtumikie Mungu kwa uaminifu anayepaswa kuwa ndiye utajiri wako pekee.

SALA: Ee Mwenyezi Mungu utusaidie kutambua kwamba Wewe ndiye tegemeo letu pekee.